Flower
Flower

Friday, May 17, 2019

FASIHI YA KISWAHILI NA NADHARIA ZA FASIHI

Balisidya (1987) anaeleza kuwa fasihi ya Kiswahili ni fasihi yoyote ambayo imeelezwa kwa Kiswahili ikiwa na lengo la kuwasilisha yasemwayo katika hadhira kubwa zaidi kuliko familia, koo, au kabila fulani na imeandikwa na wale wanaozungumza Kiswahili iwe ni lugha yao ya awali au lugha ya pili.

Mulokozi (1996) akimnukuu Mazrui na Syambo (1992) wanaeleza kuwa fasihi ya Kiswahili ni ile iliyoandikwa kwa Kiswahili tu, iwapo inazungumzia utamaduni wa Kiswahili au utamaduni mwingineo. Maadamu fasihi hiyo imetumia lugha ya Kiswahili na imefuata mbinu za ufasaha wa lugha hiyo.

Kwa ujumla fasihi ya Kiswahili ni fasihi ambayo imeandikwa kwa lugha ya Kiswahili na inazungumzia utamaduni wa waswahili na mwingineo na inaweza kuandikwa na wazawa wa lugha ya Kiswahili au mtu yeyote mwenye ujuzi wa lugha ya kiswahili. Pia fasihi linganishi imefasiliwa na wataalamu mbalimbali kama ifauatavyo;
Remak (1971) anafasili fasihi linganishi kuwa ni uwanja wa kifasihi unaohusika na uchunguzi na mahusiano ya kifasihi nje ya mipaka ya nchi moja, pia kati ya fasihi na fani nyinginezo. Katika fasili hii huonyesha kuwa fasihi linganishi hujishughulisha na fasihi na fani nyingine kama tafsiri, sosholojia na saikolojia.

Wamitila (2003) anaeleza kuwa fasihi linganishi inahusu uchambuzi wa maandishi ya wakati mmoja na aina moja na katika lugha mbalimbali kwa nia ya kumiliki sifa zinazoyahusisha kama athari, vyanzo, sifa zinazofanana na tofauti za kiutamaduni. Anaendelea kueleza kuwa inawezekana kufanya hivi kwa nia ya kuangalia matapo mbalimbali, maendeleo hata nadharia za kiuhakiki.
Kwa ujumla fasihi linganishi ni taaluma ya usomaji wa matini za tamaduni tofauti au utamaduni wa aina moja ili kubaini mazingira ambayo kazi hizo huingiliana na kutofautiana. Vilevile nadharia imefasiliwa na wataalam mbalimbali kama vile;

Massamba (2009) anafasili nadharia kuwa ni taratibu, kanuni na misingi ambayo imejengwa katika muundo wa   kimawazo kwa madhumuni ya kutumiwa kama kielelezo cha kuelezea jambo. Fasili hii inathibitisha kuwa nadharia inahusisha mawazo ambayo huwekwa kwa mpangilio maalumu ili kuelezea jambo fulani.

Amini (2005) anaeleza kuwa nadharia ni jumla ya mambo yote ambayo mtafiti amekusudia kuelezea, kuchambua, kuelewa au hata kutabiri jambo fulani kwa utaratibu maalumu.
Kwa ujumla nadharia ni mawazo, maelezo au mwongozo uliopangwa ili kusaidia kueleza, kutatua au kutekeleza jambo fulani. Vilevile dhana za historia, itikadi na utamaduni zimefasiliwa kama ifuatavyo;

Ndallu na wenzake (2014) wanafasili historia kuwa ni elimu ya mambo yaliyopita. Katika fasili hii wamejikita kueleza kuwa historia hujishughulisha na mambo mbalimbali ya kale au yaliyopita. Hivyo basi historia ni kujifunza mambo yaliyopita, yaliyopo na kutabiri yajayo.

Ndallu na wenzake (2014) wanafasili utamaduni kuwa ni desturi fulani za maisha zilizotolewa; mila na ustaarabu. Katika fasili hii wanadai kuwa utamaduni ni lazima uhusishe desturi, mila na ustaarabu. Hivyo basi utamaduni ni jinsi binadamu anavyokabili maisha katika mazingira yake. Hiyo hujumuisha ujuzi, imani Sanaa, maadili sheria na desturi ambavyo mtu anajipatia kama mwanajamii.

Ndallu na wenzake (2014) wanafasili itikadi kuwa ni mambo ya kidini ambayo muumini anapaswa kuyakubali na kuyaheshimu kuwa ni kweli. Katika fasili hii wanasisitiza kuwa itikadi hujishughulisha zaidi na masuala ya kidini yaani imani ya mtu ambayo anaamini. Hivyobasi itikadi ni mkusanyiko wa imani unaoshirikiwa na kikundi cha watu fulani. Baada ya kufafanu dhana muhimu zilizojitokeza kwenye swali letu, zifuatazo ni nadharia za fasihi linganishi na namna zilivyoathiriwa na mielekeo ya kihistoria, kitamaduni na kiitikadi.

Nadharia ya ubadilikaji taratibu, ni nadharia ya kiutandawzi iliyoasisiwa na Charles Darwin (1809-1914) katika andiko lake la Orgin of species lililochapishwa mwaka 1959. Charles Darwin ni mwana baiolojia ambaye alifanya utafiti kuhusu mabadiliko ya viumbe hai ambao waliishi miaka ya mamillioni iliyopita. Katika utafiti wake aliona njia rahisi ya kubaini chimbuko la binadamu ni kulinganisha sifa za kibiolojia baina ya viumbe hai hao. Aligundua kwamba, kama viumbe hai wanasifa zinazofanana basi viumbe hai hao wanatoka katika asili moja na wakapitia mabadiliko mbali mbali hadi kufikia hali walionayo sasa. Pia anaeleza kuwa viumbe wanaoendelea kuishi ni kwasababu wameweza kumudu mapambano dhidi ya mazingira na jambo hili aliliita Survival for the fittest. Mawazo ya utafiti wa Darwin yalishadidiwa na wanazuoni mbalimbali kama vile Edward Burnet Taylor, James Cierge Frazer, John Roscoe, Edward Smith, watafiti hawa walikuwa wanachunguza utamaduni wa binadamu. Katika utafiti wao walikusanya simulizi kutoka katika jamii mbalimbali za Afrika, Asia na America ambapo baada ya ukusanyaji wa simulizi hizo waligundua kuwa zilikuwa na ufanano wa kimaudhui. Wanaubadilikaji taratibu wanaamini kuwa masimulizi tuliyonayo sasa yanaasili moja isipokuwa yamekuwa yakibadilika kutokana na wakati, pia wanaamini kuwa viumbe wote wametoka kwenye asili moja hivyo wanaakili sawa.

Ubora wa nadharia hii ni kuwa msingi wa nadharia nyingine zilizofuatia lakini pia imesaidia kueleza asili ya masimulizi tulionayo sasa, mfano ngano. Udhaifu wa nadharia hii nikudai kuwa fasihi ya kiafrika ni masalia ya fasihi zilizotangula, pia walizingatia kipengele cha maudhui na kupuuza kipengele cha fani lakini pia walikita zaidi kueleza kufanana kwa maudhui ya masimulizi bila kuchunguza tofauti. Nadharia hii imethiriwa na mielekeo ya kihistoria, na kiitikadi. Kwa kuanza na mwelekeo wa kihistoria;

Nadharia hii imeathiriwa na mwelekeo wa kihistoria kwani historia ya viumbe hai inahusiana na mabadiliko mbalimbali ambayo wanyama wanayapitia na kuihusianisha na fasihi. Kwani kutokana na mabadiliko mbalimbali ya kihistoria yanayopatikana katika jamii vivyohivyo fasihi nayo imekuwa ikipitia vipindi mbalimbali vya mabadiliko ya kihistoria. Mathalani kazi mbalimbali za kipindi cha ujima ni tofauti na fasihi ya kipindi cha utumwa na ubepari.

Pia nadharia hii imeathiriwa na mwelekeo wa kiitikadi kwani waasisi wa nadharia hii walikuwa wakiamini kuwa bara la Afrika ni giza na halina maendeleo kabisa na ndio maana walidai kuwa fasihi ilitoka kwao na kuja kwa waafrika. Hivyo basi itikadi hii waliyokuwa nayo si ya kweli kwani Afrika walikuwa na fasihi hata kabla ya ujio wa wageni. 

Nadharia ya msambao, nadharia hii imeasisiwa na Jacob na Wilhem Grimm, baadae mawazo yao yaliendelezwa na Maxmuller pamoja na Stere Thompson kutoka marekani. Wataalam hawa wanaamini kuwa chimbuko la fasihi ni moja lakini kutokana na maingiliano ya kijamii ndio yaliyosababisha kusambaa kwa ngano hasa kutoka jamii zilizostaraabika (Ulaya) kuja katika jamii zisizostaarabika (Afrika). Okpewho (1992) anadai kuwa wanamsambao walijishughulisha na kuhusisha ngano za jamii mbalimbali na kugundua kuwa ngano hizo zinaufanano unaokaribiana sana. 
Uhusiano huu unahusishwa na kipindi cha kihistoria ambacho kulikuwa na mawasiliano baina ya jamii moja na nyingine. Katika utafiti wao wanamsambao waligawanyika katika makundi mawili, kundi la kwanza ni wale waliotoka katika shule ya India, kundi hili liliongozwa na Jacob na Wilhelm ambapo walikusanya hadithi mbalimbali katoka Ujerumani na barani Ulaya na kugundua kuwa ngano hizi zinafanana. Walihitimisha kuwa ngano za ulaya zimeonekana na rangi ya nasaba bora iliyopata kuishi huko kati ya Kaskazini na Asia rangi ya nasaba bora ni lugha zote za ulaya zinazohusishwa na rangi hiyo. Hivyo waligundua kuwa ngano zilikuwa zinasambaa na makundi ya wahamiaji. Kundi la pili ni la shule ya kifini shule hii ilianzishwa na Elias Lonnrot ambaye mwaka 1825 alianza kukusanya ngano za mashujaa katika nchi ya Fineland, akapitia maudhui yanayohusiana na akaziweka pamoja. Ubora wa nadharia hii ni;
Kuathiriana kwa jamii kunatokana na mwingiliano baina ya jamii hizo, ambapo zimeingiliana katika shughuli mbalimbali kama vile biashara, ufugaji, kilimo, uwindaji na kazi mbalimbali za kijamii.
Vilevile nadharia hii inaudhaifu ufuatao, kwanza wanamsambao wanaona kuwa fasihi ya kiafrika ni duni kutokana na kuiga kutoka fasihi ya kiulaya lakini pia walizingatia ufananano na kupuuza utofauti wa jamii na umuhimu wa tofauti hizo.

Nadharia hii imeathiriwa na mwelekeo wa kiutamaduni, kiitikadi na kihistoria, kwa kuanza na mwelekeo wa kiutamaduni nadharia hii imeathiriwa na mwelekeo huu kwani jamii mbili zinapoingiliana jamii moja huiga baadhi ya utamaduni wa jamii nyingine ka. Lakini pia nadharia hii imeathiriwa na mwelekeo wa kiitikadi kwani waasisi wa nadharia hii wanadai kuwa ngano tulizo nazo sasa zimetoka kwenye jamii zilizostarabika kuja katika jamii ambazo hazijastarabika. Walitoa madai hayo kulingana na itikadi zao walizokuwa nazo kuhusu bara la Afrika kuwa ni bara ambalo halijastarabika vilevile nadharia hii imeathiriwa na mwelekeo wa kihistoria kwani wanaeleza kuwa jamii za Afrika na Ulaya ziliwahi kuingilia na kupelekea utamaduni wa Ulaya kusambaa katika jamii za Afrika kutokana na uhamiaji.

Nadharia ya kisosholojia, TUKI (2004) wanaeleza kuwa sosholojia ni taaluma ya kisayansi inayohusu asili na maendeleo ya jamii pamoja na tabia zake. Nadharia hii imegawanyika katika mihimili mikuu miwili ambayo ni umahususi na mkazo katika utendaji. 

Kwa kuanza na umahususi nadharia hii ilikuwa mahususi zaidi kuliko nadharia zilizotangulia badala ya kujikita katika taaluma ya Sanaa jadi kwa ujumla (maumbile ya mwanadamu na utamaduni wake) kama walivyofanya wananadharia wa zamani. Nadharia hii ilijikita katika jamii pekeake baada ya kugundua dosari zilizofanywa hapo kabla, dosari hizo ni kama kutoa matamko ya juu juu na kijumla zaidi. Kwa hiyo wanasosholojia waliazimia kuchunguza kila jamii kwa wakati na nafasi yake kwa kurekodi kila kilichopatikana katika jamii husika. Miongoni mwa wataalamu waliochunguza nadharia hii ni kama Brownslow Malinowisky na Radcliffe – Brown (uingereza), walichunguza jamii mbalimbali katika visiwa vya Trobriand na Andaman. Mtalam mwingine ni Franz Boas (Marekani) alichunguza jamii za wenyeji wa Marekani. 

Wataalam wengine kutoka Afrika ni pamoja na E.E. Evans-Pritchard alifanya utafiti katika katika jamii ya Nuer (Sudan), William Boscom katika jamii ya Yoruba (Nigeria) na Marcel Griaule katika jamii ya Dogon (Burkina Faso) watalamu hawa waaliongozwa na mawazo ya kiubadilikaji taratibu. Muhimili wa pili ni mkazo katika utendaji, Tofauti na ilivyokuwa kwa wananadharia wa mwanzo ambao hawakupendelea kuangalia utendekaji wa fasihi simulizi, wanasosholojia waliweka msisitizo katika kuchunguza utendaji wa fani mbalimbali za fasihi simulizi. Kutokana na msisitizo huo imebainika kuwa fanani wa kazi ya fasihi wanaujuzi na ustadi wa kiutendaji katika sanaa husika na jambo hili limetuwezesha kuelewa kuwa katika fasihi simulizi kuna kipengele cha utendaji vilevile wamedokeza sifa za ndani za fasihi simulizi ya Kiafrika, na hiyo wao wanaona kuwa ili kujua fasihi ya kiafrika ni vyema kuangalia jamii na utendaji wa kazi husika.
Ubora wa nadharia hii ni kuona upekee wa fasihi simulizi ya kiafrika na kuona ilikuwa na dhima katika jamii mahususi. Upungufu wake ni kuwa wameshindwa kuchambua sanaa kubwa iliyomo kwenye matini chanzi nyingi za fasihi simulizi walizochunguza.

Nadharia hii imeathiriwa na mielekeo ya kiitikadi, kiutamaduni na kihistoria. Kwa kuanza na mwelekeo wa kiitikadi, nadharia hii imeathiriwa na itikadi ambapo waasisi wa nadharia hii wanaamini kuwa kila jamii ni vema ikachunguzwa pekeake ili kuweza kujua mambo mbalimbali ambayo yanapatikana katika jamii hiyo na kuitofautisha na jamii nyingine. Vilevile kwa upande wa mwelekeo wa kiutamaduni waasisi wa nadharia hii wanaona kuwa jamii zinatofautiana kiutamaduni hivyo basi hata utendaji wake ni tofauti baina ya jamii moja na jamii nyingine. Pia katika historia wanadai kuwa jamii zinapochunguzwa kwa wakati tofautitofauti huonyesha utofauti uliopo baina ya jamii hizo katikq kipindi fulani cha historia na kipindi kingine.

Nadharia ya utaifa, nadharia hii iliasisiwa na S. Adeboye, Baborola, Daniel P. Kunene na J. P Clark, ilizuka kwenye vuguvugu la kudai uhuru barani Afrika, wanautaifa wadai kuwa wananadharia wa nadharia ya ulimwengu hawakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu lugha za kiafrika, kwa kiwango kikubwa waliathiriwa na dhana za kikoloni na upendeleo wa kibepari kuwa Afrika ni bara la giza na washenzi wasiokuwa na aina yoyote ya ustaarabu na walistahili kustarabishwa na wazungu kupitia mlango wa ukoloni. Waasisi wa nadharia hii wanadai kuwa ni kosa kubwa kufanya utafiti bila kuwahusisha wahusika wa eneo la utafiti hivyo ili kufahamu vyema historia ya fasihi simulizi ya kiafrika ni lazima kuhusisha wataalamu na wanazuoni wa taifa au jamii hiyo kwasababu wataalam hawa ndio wenye ujuzi wa lugha, utamaduni na historia ya jamii hiyo. Kwa ujumla wanautaifa wanamini kuwa chimbuko la fasihi simulizi ya kiafrika inapatikana ndani ya jamii ya kiafrika na ili kuchunguza fasihi ya jamii husika ni sharti watalaamu na wanazuoni wajamii hiyo wahusishwe. Ubora wa nadharia ni kuhusisha wazawa wa jamii husika.

Nadharia hii imeathiriwa na mielekeo ya kiitikadi, kiutamaduni na kihistoria. Kwa kuanza na mwelekeo wa kiitikadi waasisi wa nadharia hii wanadai kuwa wakoloni walipokuja Afrika walikuwa na itikadi yao ya kibepari hivyo ilipelekea wao kutoa mawazo kuwa Afrika ni bara duni. Kwa upande wa kiutamaduni waasisi wa nadharia hii walisisitiza kuwa ni vema kuwashirikisha wataalamu na wanazuoni wa jamii husika kwani wao ndio wanajua lugha husika kwa ufasaha zaidi. Vilevile katika upande wa historia waasisi wanadai kuwa ni vema kuwa husisha wataalamu ili kuweza kufahamu vizuri historia ya jamii husika.

Nadharia hulutishi, nadharia hii iliasisiwa na wanazuoni wa kiafrika wenye mtazamo kuwa hata wageni wamechangia sana kukuza taaluma ya fasihi ya kiafrika. Wananadharia hawa wanaona kuwa fasihi ya kigeni na kijadi zimeathiriana na kuingiliana. Miongoni mwa waasisi na watetezi wa nadharia hii ni pamoja na M.M Mulokozi, Johnson, Ngugi Wa Thiong’o, Chinua Achebe, Frantz Fanon, Abiola Irele. Hivyo historia ya fasihi simulizi ya kiafrika inaweza kujadiliwa kwa kuhusisha au kuchanganya mawazo ya wataalamu wote wa kigeni na kijadi. Wao walianza kuandika kazi ya fasihi ambazo zinajaribu kuhusianisha ujadi wa waafrika na usasa unaotokana na ujio wa wageni. Mathalani Chinua Achebe katika vitabu vyake vya Things Fall Apart na No Longer at Ease na Ngugi Wa Thiong’o katika The Grain of Wheat. Mtazamo huu umekuwa maarufu na kwa kiasi kikubwa na kwa kiasi kikubwa unatumika.
Nadharia hii imeathiriwa na mielekeo ya kiitikadi, kiutamaduni na kihistoria. Kwa kuanza na mwelekeo wa kiitikadi waasisi wa nadharia hii wanaamini kuwa wataalamu wote yaani wageni na wenyeji wanamchango mkubwa katika kuiendeleza fasihi. Pia katika utamaduni wanaeleza kuwa fasihi ya kigeni na fasihi ya kijadi zimeathiriana, hivyo jamii mbili zinapoingiliana jamii moja huchota vipengele vya kiutamaduni kutoka katika jamii nyingine. Vilevile katika historia wanaeleza kuwa historia inaweza kuelezewa kwa kuzingatia mwingiliano wa jamii hizi.
Kwa ujumla nadharia za fasihi linganishi zinamchango mkubwa katika maendeleo ya fasihi ya Kiswahili kwani husaidia kujua historia ya fasihi tuliyonayo sasa, pia huwaongoza watafiti wakazi mbalimbali za fasihi pindi wanapofanya utafiti unaohusiana na fasihi simulizi na fasihi andishi, vilevile vigumu kuelezea nadharia za fasihi linganishi bila kuhusianisha na mielekeo ya kihistoria, kiitikadi na kiutamaduni kwani mielekeo hii imeathiri mno nadharia za fasihi linganishi.















MAREJELEO.
Balisidya, N. M. “Adopted or adapted to Neo Swahili Oral Literature in Tanzania” katika Kiswahili Vol. 54/1 na 54/2 (1987), Dar es Salaam: TUKI.
Massamba, D. P. D (2009) Kamusi ya Falsafa ya Lugha. Dar es Salaam: TUKI.
Mulokozi, M. M. (1996). Fasihi ya Kiswahili. Dar es salaam. DUP.
Ndallu, A. E, Babusa, H na Mirikau, S.A (2014). Kamusi teule ya Kiswahili. Nairobi- Kenya:
                                                                                Prinywell Industries Limited.
Okpewho, I. (1992). African Oral Literature. Backgrounds, Character and Contiunity. USA:
                                  Indiana University Press.
Remak, H. H. (1971). Comperative Literature: Its definition and F unction. Carbondale: Southern
                                    Illinois. 
TUKI, (2004) “Kamusi ya Kiswahili sanifu”. Dar es salaam; Oxford University Press.
Wamitila, K. W.  (2003), Kamusi ya Fasihi na Nadharia. Focus Publications Ltd.    


No comments:

Post a Comment

syliverymanyama@gmail.com

AddToAny