Flower
Flower

Thursday, February 6, 2020

Makundi ya Ufeministi

Samsoni (2017) akiwanukuu  Luvenduski & Randall (1993)  anaeleza kuwa, ufeministi ni neno la Kilatini ‘femina’ yaani wa ‘kike’ au mwanamke. Wanaendelea kwa kusema kuwa, katika lugha ya Kifaransa ‘feminisme’ linamaanisha harakati za ukombozi wa wanawake. Ni jina linalojumuisha aina nyingi za misimamo, itikadi na matapo tofautitofauti yanayochangia lengo kuu la kutetea haki za wanawake dhidi ya ubaguzi wa kijinsia uliotawala dunia kwa muda mrefu sana katika upande kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni, kidini na kijamii kwa ujumla.

Miongoni mwa wadau waliochangia kuendelea kwa kasi ya ufeministi ni Andew Dworkin mwaka 1976 huko London Uingereza, alitoa mapendekezo makali katika kukomesha utawala wa mwanaume dhidi mwanamke, kwa madai kuwa, “ili kufanikisha, tunahitaji kubomoa kabisa muundo wa mihimili ya utamaduni wa jamii kama vile sanaa, kanisa, sharia, kaya zinazodhibitiwa na baba, jamii na taswira zote za asasi, mila na desturi zilizomwona mwanamke kama mtu hovyo.”. Ithibati za kimaandishi za kifeministi zenye utaratibu na zilizoweka misingi ya nadharia ya ufeministi ni andiko la Mary la Mary Wollstonecraft linaloitwa ‘A vindication of the Right of
Women’ la mwaka (1792), andiko la Woolf liitwalo ‘A Room of One’s Own’ la mwaka (1929). Mary Wollstonecraft ndiye mwandishi aliyeasisi mazungumzo kuhusu masuala ya wanawake na kulalama kuhusu hali waliyokuwa wanapitia wanawake katika jamii. Katika miaka ya 1960, ufeministi ulishika kasi. Kwa mfano mwandishi wa kifaransa, Simone de Beauvoir katika andiko lake la ‘The Second Sex’ la mwaka 1952, anaonesha harakati za kushambulia na kukosoa baadhi ya asasi zinazochangia kumdhalilisha na kumdunisha mwanamke kama vile dini, ndoa na utamaduni. 
Semone de Beauvior, anaeleza kuwa, asasi ya ndoa inamgandamiza mwanamke kwa kumuona kama chombo cha kukidhi haja ya mwanaume na kutoa suhuhisho la kuipa kisogo asasi hii. Pia, anaeleza katika utamaduni kuwa, ni asasi inayomgandamiza mwanamke na ndiyo inayomkuza mwanamke. Kwa kuwa utamaduni ndiyo unaomkuza mwanamke, ndiyo ulioweka misingi ya kumfanya mwanamke kuwa ni kiumbe duni, na kumfanya akiukubali mfumo huu hasi.
Mwanaitifaki wengine ni Milet katika kitabu chake cha ‘Sexual Politics’ anawakosoa vikali baadhi ya waandishi wa kiume wanaoandika kazi zao zinazowasawili wanawake katika hali hasi. Alienda mbali zaidi mpaka kwa kuwashambulia wanaitifaki wa nadharia ya Saikolojia Changanuzi, ambao muasisi wake ni Freud Sigmund, wanaodai kuwa mwanamke huanza kujichukia pale anapoona kuwa yeye si wa jinsi ya kiume ambapo wao waliona kuwa ni wivu wa zuba.

Wamitila (2003:253) anaeleza kuwa, ufeministi ni msingi na msukumo mkubwa pamoja na nia ya kupigania ukombozi wa mwanamke kutokana na pingu za kiutamaduni, kidini, kijamii, kisiasa na kiuchumi. Fasili hii inadadisi itikadi ya kiume ambayo imekuwepo katika jamii kwa kipindi kirefu pamoja na mikabala ya kiubabe dume. 

Njogu na Chimerah (2008:18) anaeleza kuwa, ufeministi au mtazamo kike ni nadharia inayokinzana na mikabala ya kiumeni inayoonekana kupendelea wanaume na kuwanyanyasa wanawakae. Mtazamo huu unaonesha namna wanaume wanavyowakandamiza wanawake na kuwasahau kuwa wote wanahitaji kupata haki sawa katika nyanja za kiuchumi, kisiasa, kijamii na kiutamaduni.

Cambridge Dictionary (1995) wanaeleza kuwa ufeministi ni mtazamo wa kiimani ambao wanawake wanatakiwa wawe na haki sawa, nguvu na nafasi kama ilivyo kwa wanaume na kutazamwa kwa usawa. Katika fasili hii hailezi kuwa, njia gani zitumike kuwapa wanawake haki sawa kama walizonazo wanaume.

Mulokozi (2017:368) anaeleza kuwa, ufeministi ni vugu vugu na itikadi ya mapambano ya mwanamke ya kujikomboa kutoka katika mikakati ya kunyonywa, kukandamilzwa na kubaguliwa ndani ya jamii, pamoja na itikadi za ubaguzi zinazoambatana na hali hiyo.
Kwa ujumla, ufeministi ni michakato ya itikadi ambayo inalenga kutafuta na kufikia usawa kati ya wanawake na wanaume katika nyanja zote za kimaisha kama vile kisiasa, kielimu, kijamii kiutamaduni na kiuchumi. Hivyo ufeministi ni itikadi ambayo inapigania usawa kwa jinsi zote.

Wamitila (2003) anaeleza kuwa, historia ya ufeministi inadai kwamba, mapambano ya wanawake dhidi ya wanaume (ufeministi) yalianza karne ya 19. Mapambano haya yalichukuliwa kama harakati za kudai haki za wanawake yaliyoanzia Ulaya. Miongoni mwa haki hizo, ni pamoja na haki ya kupiga kura kwenye chaguzi za siasa, haki ya kumiliki na kupata elimu. Wakati, Mulokozi (2017:368)) anaeleza kuwa, ufeministi ulianza Ulaya na Marekani mnamo karne ya 18, wafeministi na watetezi wengine wa wanawake walibainisha baadhi ya mambo na asasi zinazomkandamiza mwanamke, zikiwemo mila na desturi, ndoa, dini na mifumo ya kiuchumi na kisiasa. Kwani haki za binadamu zilipoanza kufanya kazi hapo awali zilijadiliwa kwa wanaume pekee.

Hivyo, baada ya harakati za kumkomboa mwanamke kutoka katika ugandamizwaji na unyonyaji dhidi ya mwanaume, ndipo yalipozuka makundi ya ufeministi kama ifuatavyo;
Wafeministi wanamapokeo (ki marx), kundi hili linaangalia kwamba, uhusiano wa kisiasa kati ya mwanamke na mwanaume si sawa ingawa, wanawake hawapaswi kuvuruga mfumo uliopo (wa kiugandamizaji). Miongoni mwa waasisi wa kundi hili ni pamoja na Selma Jems, Angela Davis, Crala Fraser, Raya Dunayevisk Shulamith Firestone na Heidi Hartmann.

Wanamapokeo ni tapo linalodai kuwa ugandamizaji wa mwanamke umetokana na mfumo wa unyonyaji wa kibepari, mfumo ambao umeigawa jamii katika makundi makuu mawili, tabaka la wasionacho na walionacho. Kwa mujibu wa wanaitifaki hawa, asilimia kubwa ya tabaka la wasionacho ni wanawake ambao wapo chini ya wanaume kutokana na mfumo dume unaowapa hadhi wanaume. Mfumo huu wa kibepari unawapa fursa watu wachache kumiliki mali ambao waliowengi ni wanawake. 

Kundi hili linadai kuwa, ili mwanamke aweze kukombolewa na awe na uhuru wa kutokugandamizwa, ni lazima ubepari utokomezwe, ili kutoa fursa kwa jinsi zote mbili katika jamii. Kwa mujibu wa Malenya (2012) Karl Marx na Engels walikuwa wakiamini kuwa, familia ndiyo taasisi ya kwanza ya kijamii ambako hakuna usawa kati ya mwanamke na mwanaume na kwamba mfumo huo unapaswa kuangamizwa na badala yake zianzishwe taasisi za ushirika au ujima ili kazi za nyumbani zifanywe na jinsi zote mbili kwa usawa.

Hivyo wafeministi wanamapokeo wanapigania haki sawa ambazo zimekosekana kutokana na mfumo kibepari wa unyonyaji na ukandamizaji unaofanywa na tabaka tawala ambalo wahusika wengi ni wanaume dhidi ya tabaka tawaliwa ambao walio wengi ni wanawake, ili kuleta usawa kati ya wanaume na wanawake katika nyanja zote za kijamii kuanzia ngazi ya familia, kijamii hadi kitafa kwa maendeleleo endelevu yasiyo na ubaguzi.  

Wafeministi huru (Liberal feminism), ni kundi lililoanzia mwishoni mwa karne 19 na mwanzoni mwa karne ya 20 katika harakati za kupigania uhuru wa mwanamke katika kufanya maamuzi bila kuingiliwa na mwanaume. Waasisi wa kundi hili ni pamoja na Marry Wollstonecraft, Judith Surgent 

Murray, Frances Wright. Wanafalsafa wa kundi hili wanatetea usawa kati ya mwanamke na mwanaume katika nyanja za kisiasa, kielimu, kiuchumi na kiutamaduni ambao ulishika kasi miaka ya 1960 katika harakati za makundi ya kudai haki dhidi ya ubaguzi wa rangi na ubaguzi wa kijinsia. 
Waitifaki hawa, wanadai kuwa, binadamu wote ni sawa wake kwa waume, hivyo, wanawake nao wana haki ya kuwa huru katika kuyatekeleza majukumu na malengo yao, yaani kupewa fursa ya kuamua ni wakati gani wa kuwa na watoto bila shinikizo la wanaume zao, pia wanatilia mkazo katika suala la malezi kuwa ni la wote mwanamume na mwanamke. Wanaitifaki hawa wanaangalia kuwa, mgawanyo wa kazi kutokana na hali ya kijinsi kati ya mwanamke na mwamume si sawa, hivyo unapaswa kubadilishwa na kwamba, kama mwanamke anafanya kazi za ndani azifanye, lakini kama atamua kufanya shughuli nyingine za kijamii nazo afanye, na ana uhuru wa kutoa mimba na kuzaa. 
Misingi ya wafeministi huru ni kwamba, mfumo uliopo unapasawa kubadilishwa.
Pia kundi hili linatoa mwongozo kwa jamii kuwa, mwanamke anapaswa kuwa huru katika nyanja zote za uzalishaji mali ili kuwe na usawa kati ya mwaume na mwanamke, kuliko kumwacha mwanaume atawale katika nyanja zote na kunyima mwanamke fursa ya uzalishaji mali katika jamii. Mfumo gandamizi wa kibepari ndiyo unaowapa nafasi wanaume kuwakandamiza wanawake, hivyo unapaswa kuondolewa ili kuleta usawa kawa jinsi zote mbili katika uhuru wa kufanya mambo.

Wanamapinduzi (Radical feminism) hili ni kundi la kimapinduzi, linalopinga mfumo dume na kudai kwamba, unapaswa kutupiliwa mbali. Kundi hili linahusisha makundi mbalimbali ya kudai haki ambayo yalishika kasi zaidi miaka ya 1960. Miongoni mwa waasisi wa kundi hili ni Ellen Wills, Ti-
Grace Atkson, Carol Hanisch, Judith Brown na Shulamith Firestone. Waitifaki hawa wanadai kuwa huu ni mfumo wa kibepari unaoendeleza unyonyaji na ugandamizaji wa mwanamke katika nyanja za kisiasa, kiuchumi. kiutamaduni na kielimu. 
Kundi hili linadai haki sawa katika masuala ya uongozi kwa jinsi zote mbili, kiume na kike. Kwa kuwa jamii nyingi zimemnyima mwanamke kushiriki kufanya maamuzi kuanzia ngazi ya familia, kijamii na kitaifa, hapo ndipo kundi hili lilisimama kidete katika kudai usawa katika suala la maamuzi. Jitihada hizi za kuitaka jamii impe fursa mwanamke katika kufanya maamuzi, zilizaa matunda katika mkutano wa Beijing wa mwaka 1995 wakati huo Balozi Getrude Mongela, ukihudhuriwa na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa. 
Katika mkutano huu, maazimio kadha wa kadha yalipitishwa ikiwa ni pamoja na wanawake kutengewa viti maalumu bungeni, msukumo ambao uliwafanya wanawake kuwa na fursa katika kufanya maamuzi, hatua ambayo ilizaa matunda kwa wanawake kupata nyazifa katika mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali hivyo kuleta usawa kwa kuwa na uhuru wa maamuzi kwa wanawake na wanaume katika jamii.

Wafeministi wa kijamaa (socialist feminism), hili ni kundi lililoshika kasi miaka ya 1960 na 1970, ambalo linaeleza kuwa, uhusiano baina ya wanawake na wamaume unaotokana na muundo wa kijamii na kiuchumi na mageuzi makubwa katika jamii, na kwamba kuwepo kwa haki sawa kati ya wanawake na wanaume kupo katika usawa wa kijamii na kufutwa kwa dhulma ya kijinsia na kitabaka katika jamii. Miongoni mwa waasisi wa kundi hili ni pamoja na Heather Booth, Day Creamer, Susan Davis, na Tobey Klass. Wafeministi wasoshalisti wanakubaliana na uchambuzi wa wenzao wa kimaksi kuhusu uhusiano wa kitabaka wa ubepari ambao umekuwa gandamizi kwenye jamii kwa kuifanya jinsi ya kike kuwa ndiyo inayoathirika kwa kiasi kikubwa. 
Gabriel (2010) anaeleza kuwa, wafeministi wa kijamaa wanadai kuwa, ili kuwe na usawa kati ya mwanamke na mwanamume, ni lazima kuwe na mapambano dhidi ya mfumo dume na ubepari, na mapambano hayo yanapaswa kuanzia sehemu za viwandani hadi kazi zote za umma na binafsi, kiutamaduni ambako ndiko wanawake  wanabaguliwa ili kuleta usawa wa kijinsia kwa wanaume na wanawake. Wanadai kuwa kuleta usawa wa kijamii kati ya wanawake na wanaume, mfumo dume unapaswa kuondolewa ili kuwe na mgawanyo sawa kimajukumu na njia za uzalishaji mali na kushika nafasi mbali mbali ambazo wanawake na wanaume watanufaika kwa pamoja.

Ufeministi wa kiutamaduni, hili ni kundi ambalo linautizama utamaduni kama nyenzo kubwa katika kumfanya mwanamke aamini hali aliyonayo. Kwa mfano; kukandamizwa, kudhalilishwa na kukosa uhuru wakutoa maoni. Ni kundi ambalo linatoa wito kwa wanawake wote kuona umuhimu na wajibu wa kushiriki katika ukombozi wa mwanamke dhidi ya mila na desturi zinazowagandamiza. Wanaharakati wa kundi hili ni kuwakomboa wanawake kutoka katika minyororo ya utamaduni unaowanyima fursa za kufanya maamuzi, kuotoa maoni na kutoshiriki badhi ya shughuri ambazo jamii huwaona wao ni kama chombo tu ambacho hakina nafasi yoyote isipokuwa kumsikiliza mwanaume nah ii ni kutokana na mfumo uliopo katika jamii nyingi.

Wafeministi wasagaji, ni wanaharakati walioibuka miaka ya 2000 na kuendelea. Wafuasi wa kundi hili wanamchukulia mwanaume kuwa ndiye adui namba moja kwa mwanamke, hivyo mwanaume hawezi kushiriki katika harakati za kumkomboa mwanamke. Waitifaki wa kundi hili, pia hudai kuwa wanaume hutumia asasi ya ndoa kumkandamiza mwanamke, asasi ambayo mwanamke huchukuliwa kama chombo tu katika familia, ni mtu ambaye hana majukumu mengine Zaidi ya kulea familia, ni mtu ambaye thamani yake haionekani Zaidi ya kuwa chini ya mamlaka ya mwaume katika maamuzi na kumiliki nyanja zote za uzalishaji mali. Aidha kundi hili linadai kuwa, uhuru wa mwanamke utapatikana pale atakapoacha kujamiiana na mwanamume badala yake washirikiane wao kwa wao hata katika masuala ya kimapenzi. 

Kwa kuhitimisha, wafeministi wanaamini kuwa mtazamo wa jamii nyingi dhidi ya wana nb wake ni kudunisha na kuwafanya watu wa daraja la pili. Kwa msingi huo wanasistiza juu ya kubadilishwa mtazamo wa jamii kuhusu wanawake na kufuta ubaguzi dhidi yao, mtazamo ambao umesababisha kupatikana kwa baadhi ya mafanikio makubwa kwa maslahi ya wanawake wa nchi za magharibi, ingawa Irib (2014) anadai kuwa, suala la kupambana na ubaguzi huo halipaswi kuwa kisingizio cha kutokomeza na kuua maana ya maisha, kumdumisha mwanamume katika jamii na kulazimisha haki na majukumu sawa na yanayofanana licha ya tofauti za kimaumbile.

                                                                      MAREJELEO
Cambridge (1995) Andvanced Leaners English Dictionary: London. Cambridge University Press
Gabriel, G. (2015) Ufeministi, Itikadi na Misingi yake. Mwanza: Serengeti Publishers.
Irib, World Service (2014) Matatizo ya Wanawake katika Ulimwengu wa Magharibi.
            http://www.kiswahili.irib.ir/38823
Malenya, M. M. (2012) Matumizi ya Lugha katika Fasihi Simulizi. Mwanza. Inland press.
Mulokozi, M.M. (2017) Utangulizi wa Fasihi ya Kiswahili: Dar es Salaam: Moccony Press.
Njogu K & Chimerah. (1999) Ufundishaji wa Fasihi. Nadharia na Mbinu. Nairobi: Jomo 
            Kenyatta Foundation.
Samson, M. K. (2017) Nadharia ya Ufemisti Katika Jamii: St. Augustine of Tanzania. Mwanza 
TUKI (2012) Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es Salaam. TUKI.
Wamitila, K.W. (2003). Kichocheo cha Fasihi Simulizi na Fasihi Andishi. Nairobi: Focus 
                                                 Publication Limited.


No comments:

Post a Comment

syliverymanyama@gmail.com

AddToAny