Flower
Flower

Saturday, February 29, 2020

Matini za tafsiri


0.1    Utangulizi
Sehemu ya kwanza ni utangulizi ambapo tumejadili dhana ya matini, tafsiri na matini za tafsiri, sehemu ya pili ni kiini cha swali ambapo tumejadili vigezo anuai na umuhimu wa uanishaji wa matini za tafsiri, sehemu ya tatu ni hitimisho na ya nne ni marejeleo.
2.0 FASILI YA MATINI, TAFSIRI NA MATINI ZA TAFSIRI
Katika sehemu hii tumetoa fasili ya matini, tafsiri na matini za tafsiri kama ilivyofasiliwa na wataalamu mbalimbali:
2.1 Dhana ya Tafsiri
Wataalamu mbalimbali wamefasili dhana ya tafsiri kama ifuatavyo;
Catford (1965:20) anafasili tafsiri ni kuchukuwa mawazo yaliyo katika maandishi kutoka lugha moja (lugha chanzo/ LC) na kuweka badala yake mawazo yanayolingana na hayo kutoka lugha nyingine (lugha lengwa/ LL).
Nida na Taber (1969) tafsiri ni uzalisha upya ujumbe wa lugha chanzo kwa kutumia visawe asili vya lugha lengwa (LL) vinavyokaribiana zaidi na lugha chanzi, kwanza kimaana pili kimtindo.
TUKI (2002) tafsiri ni kutoa mawazo kutoka katika lugha moja kwenda lugha nyingine bila kubadilisha maana.
Kwa ujumla, tafsiri ni uhawilishaji wa mawazo au ujumbe au taarifa iliyopo katika maandishi kutoka lugha chanzo kwenda lugha lengwa bila kupoteza maana ya matini asilia.
2.2 Dhana ya Matini
Mwansoko (1996) anafasili matini ni wazo au mfululizo wa mawazo wenye utoshelevu wa kimaana ambao unahitaji kutafsiriwa. Mfano matini yaweza kuwa neno, kirai,kishazi, sentensi, aya au tungo.
Massamba (2009) amefasili matini kuwa ni maelezo ya kitu ambayo ama yameandikwa na mtu au yamenukuliwa na ambavyo yamekusudiwa kutumiwa kwa madhumuni maalumu.
TUKI (2013) matini ni kifungu cha habari kilichoandikwa. Fasili hii inaweka bayana juu ya habari ambayo ipo katika maandishi, hivyo maelezo yaliyo katika maandishi ni matini ambayo yanaweza kuwa ni ya aina mbalimbali kama vile matini ya kisiasa.
Kwa ujumla matini ni wazo au mawazo yenye utoshelevu kimaana yaweza kuwa katika maandishi au yasiwe katika maandishi bali matini inayotafsiriwa lazima iwe katika maandishi.

2.3 Dhana ya Uainishaji wa Matini za Tafsiri
Florence (2014:24) anaeleza kuainisha matini ni kuzigawa au kuziweka matini katika makundi mabalimbali kwa kuzingatia kufanana kwake kwa sifa kadhaa, anaendelea kueleza kuwa sababu za kuanisha matini za tafsiri ili kupata aina au makundi kadhaa yatakayo tuongoza kuchagua njia au mbinu ya kutafsiri.
3.0 vigezo vya  uanishaji wa matini za tafsiri
Florence (2014:24) ameainisha vigezo vitatu vya uainishaji wa matini za tafsiri ambavyo ni kigezo cha mada, kigezo cha istilahi na kigezo cha dhima kuu za lugha.
3.1 Kigezo cha Mada/ Maudhui
Katika kigezo hiki kinachoangaliwa ni kwamba matini inaongelea nini au inahusu nini kwa mtazamo wa kijumla. Kwa kutumia kigezo hiki cha mada tunapata aina tatu za matini ambazo ni matini za kifasihi, matini za kiasasi na matini za kisayansi.
3.1.1 Matini za Kifasihi
Ni matini zinazohusu maandiko ya kifasihi kama hadithi fupi na riwaya, tamthiliya, ushairi na kuendelea. Mfano tamthiliya ya Mfalme Edipode iliyotafsiriwa na Samwel Mushi na Mabepari wa Venusi iliyotafsiriwa na Mwl. J. K Nyerere.
3.1.2 Matini za Kiasasi
Ni matini zinazohusu siasa, biashara, fedha, sheria, serikali na asasi zinginezo. Kwa mfano matini hizi za kimamlaka ni kama vile matini za kisiasa na serikali (hotuba, risala, mikataba na vyeti).
3.1.3 Matini za Kisayansi
Ni matini zinazojumuisha nyanja zote za sayansi na teknolojia. Mfano maelekezo ya matumizi ya vifaa mbalimbali vya kielektroniki. Mfano matini za Kamusi za Sayansi kama vile baiolojia, fizikia na kadhalika.
3.2 Kigezo cha Matumizi ya Istilahi
Florence (2014) Kigezo hiki huangalia kiwango cha matumizi ya istilahi za uwanja fulani. Hivyo matini huainishwa kwa kuangalia wingi au idadi za istilahi au msamiati maalumu kwa ajili ya taaluma husika. Kwa kuangalia idadi ya istilahi tunapata aina tatu za tafsiri ambazo ni  matini za kiufundi, nusu ufundi na matini zisizo za kiufundi.

3.2.1 Matini za Kiufundi
Hizi ni matini ambazo huwa na idadi au matumizi makubwa ya istilahi.
3.2.2 Matini za Nusu Ufundi
Ni aina ya matini ambazo huwa na kiwango cha kati cha matumizi ya istilahi.
3.2.3 Matini Zisizo za Kiufundi
Matini hizi zinakuwa hazina matumizi ya istilahi na hivyo hutumia msamiati wa kawaida.
3.3 Kigezo cha Dhima Kuu za Lugha
Bulher (1965), akinukuliwa na Mwansoko (2013:11), ameainisha dhima kuu za lugha tatu ambazo ni dhima elezi (expressive function), dhima arifu (informative function) na dhima amili (Persuasive function).
3.3.1 Dhima Elezi
Dhima elezi, amabapo lugha hutumiwa kwa madhumuni kueleza hisia za mtu binafsi bila kujali hadhira. Kiini cha dhima elezi ni mwandishi.
3.3.2 Dhima Arifu
Dhima arifu, ambapo lugha hutumiwa kama nyenzo ya kutolea taarifa. Kiini cha dhima arifu ni ukweli.
3.3.3 Dhima Amili
Dhima amili, hapa lugha hutumiwa kwa madhumuni ya kuibua au kuchochea hisia za hadhira. Kiini cha dhima amili ni hadhira.
4.0 UMUHIMU WA UAINISHAJI WA MATINI ZA TAFSIRI  
Ufuatao ni umuhimu wa uainishaji wa matini za tafsiri kama ulivyo jadiliwa na wataalamu mbalimbali.
4.1 Mahususi ya Matini ndiyo Inayoukilia Mbinu Mwafaka ya Tafsiri
Mwansoko (1996:15) anaelezea kwa kutoa mfano kuwa, mahususi ya matini ndiyo inayoukilia mbinu mwaka ya tafsiri mfano matini amili huwa na muelekeo wa kutafsiri zaidi kwa kutumia tafsiri ya kimawasiliano(tafsiri huru). Hivyo uanishaji wa matini za tafsiri ni muhimu kwani mfasiri huweza kukilia mbinu mbalimbali kutokana na matini husika.

4.2 Urahisisha Upangaji wa Gharama
Mwansoko (1996:15) anaendelea kwa kutoa umuhimu mwingine wa uanishaji wa matini za tafsiri kuwa uanishaji wa matini za tafsiri humsaidia mfasiri kupanga gharama za matini mbalimbali, mfano bei za matini za kisayansi hutofautiana na bei za matini za kisheria hivyo gharama za kufasiri matini hupangwa kulingana na aina ya matini inayofasiliwa. Pia humsaidia mfasiri kujua atatumia muda gani katika kufasili matini.
4.3 Hurahisisha kazi ya kufasiri Matini
Mwanjala (2011:177) anaelezea pia umuhimu mwingine wa kuanisha matini za tafsiri kuwa, uanishaji wa matini za tafsiri humsaidia mfasiri kurahisisha kazi ya kufasiri kulingana na aina ya matini, mfano tafsiri zinazohusisha matini zisizo za kiufundi ambazo huwa hazina matumizi ya istilai na hivyo kutumia msamiati wa kawaida urahisi wa kutafsiri ni tofauti na urahisi wa kufasiri matini nyingine mfano matini za kisayansi.
4.4 Uainishaji Unamsaidia Mfasiri Kuandaa Zana za Kufasiri
Mwanjala (2011:177) anaendelea kwa kueleza umuhimu mwingine wa uanishaji wa matini za tafsiri kwa kusema uanishaji huu humsaidia mfasiri kuandaa zana mbalimbali zinazotumika katika kazi ya kutafsiri. Mfano wa zana ni kamusi, karatasi, kalamu na rula hivyo umuhimu huu msaidia mfasiri kutafuta zana kabla ya kuanza kufasiri mfano mfasiri anataka kufasiri matini za kisanyansi hapa mfasiri hana budi kutafuta kamusi mbalimbali za kisanyansi ili aweze kifanikiwa katika kazi yake.
4.5 Uainishaji Humsaidia Mfasiri Kuteua Mbinu ya Kufasiri Pamoja na Nadharia Faafu kwa Mujibu wa Aina ya Matini
Mwanjala (2011:177) anaeleza  umuhimu mwingine wa uanishaji wa matini kuwa matini kama vile matini za kisanyansi hufasiliwa vyema zaidi kwa kutumia tafsiri maana ilihali matini amili hufasiliwa zaidi kwa kutumia tafsiri mawasiliano, utofauti huu umetoka na umuhimu wa uanishaji ambapo humsaidia mfasiri kuteua mbinu na nadharia mbalimbali zitakazo muongoza katika kazi yake ya kutafsiri.
 4.6 Uainishaji Matini Hutoa Muongozo Kuhusu Kiwango cha Ugumu wa Kufasiri kwa Mujibu wa Matini Husika.
Mwanjala (2011:177) kwa upande mwingine Mwanjala anamalizia kwa kuelezea umuhimu mwingine wa uanishaji wa matini ambapo, uanishaji huu wa matini za tafsiri humsaidia mfasiri kujua kiwango cha ugumu ambapo huweza kusababishwa na muda pamoja na gharama atakazozihitaji katika kufasiri kila aina ya matini kwani matini. Mfano za kisanyansi muda na gharama ni tofauti na muda na gharama zitakazotumika  katika kufasiri matini nyingine mfano matini zisizo za kiufundi na hivyo viwango vya ugumu baina ya matini moja na nyingine hutofautiana.
5.0 Hitimisho
Kwa kuhitimisha uanishaji wa matini za tafsiri ni muhimu kwa mfasiri yeyote katika kukamilisha kazi za tafsiri kwani vigezo anuai vya uanishaji wa matini ndio msingi matini bora kwa mfasiri. Pia mfasiri huweza kutumia kigezo zaidi ya kimoja katika kutafsiri matini lengo ni kufanya kazi bora. Hivyo  haina budi kuzingatiwa katika kazi ya kufasiri.


                                                                    6.0 Marejelo
Catford, J.C. (1965). A linguistic Theory of Translation. London: OUP
Florence, A.M (2014). Tafsiri na Ukalimani ( Hakijachapishwa).
Nida, E.A na Taber, C. R (1969). The Theory and Parctice of Translation. Prentice Hall: London
Massamba, D.P.B. (2009. Kamusi ya Isimu na Falsafa ya Lugha. Dar es Salaam: TUKI
Mwansoko na wenzake (2013). Kitangulizi cha Tafsiri. Nadharia na Mbinu, Dar es Salaam:
                                       TUKI
Mwansoko, H.J.M. (1996). Kitangulizi cha Tafsiri. Nadharia na Mbinu. Dar es Salaam: TUKI
TUKI (2013). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es salaam: TUKI
Wanjala, F.S, (2011). Misingi ya Ukalimani na Tafsiri. Mwanza: Serengeti Educational
                      Publishers LTD












No comments:

Post a Comment

syliverymanyama@gmail.com

AddToAny