UTANGULIZI
Wataalam
mbalimbali wamefasili dhana ya utendi kama ifuatavyo:
Mulokozi
(1983:13, 1996:85) anasema utendi ni ushairi wa matendo. Ni utungo mrefu wenye
kusimulia matukio ya kishujaa yenye uzito wa kijamii au kitaifa. Matukio haya
huweza kuwa ya kihistoria lakini tendi nyingi huchanganya historian a visakale
au visasili
Wamitila
(2003:333) yeye anasema utendi huelezea shairi refu la masimulizi kwa mapana
linalohusu matendo ya mashujaa. Utendi unahusisha hadithi za kishujaa, visasili
na hata chimbuko la taifa Fulani. Ameendelea kubainisha aina mbili za utendi
simulizi na utendi andishi
Fasili
ya Wamitila na Mulokozi kuhusu dhana ya utendi zinafanana kwa kuwa wote wanaihusisha na matendo, matukio ya kishujaa
na utaifa, bali kilichoongezwa ni kubainisha aina za tendi ambazo ni tendi
simulizi na andishi.
Kwahiyo
utendi ni kama makavazi ya jadi ya historia ya jamii Fulani ambayo kupitia
tendi mbalimbali jamii inajitambua kuhusu historia yake katika vipindi
mbalimbali ilimopitia chimbuko lake, mashujaa wao na kujua mila na desturi zao.
Baadhi ya tendi zijulikanazo ulimwenguni ni Utendi wa Fumo Liyongo, Kachwenyanja,
Rukiza, Mugasha, NyakiiruKibi (Afrika Mashariki), Sundiata (Mandingo-Afrika ya
kati), Gilgamesh(wa-kisumeri), Nibelungenlied(Ujerumani), Ramayana na
Mahabarata(India), Jumong(Korea), Kalevalaa(Ufini) na Hamziyyah(Misri). Kazi
hii itajikita zaidi kuelezea utendi wa Hamziyya.
Utenzi
wa Hamziyya ni utungo wenye asili ya kiarabu, uliotungwa na Muhammad bin Said
Al-Busiri na kutafsiriwa kwa Lugha ya Kiswahili na Sharrif Aidarus. Utendi huu
ni tafsiri ya zamani sana katika lugha ya Kiswahili ingawa kitarehe kuna kazi
zilizoitangulia katika kutungwa kwake kama vile utenzi wa Tambuka (Chuo Cha
Herikali)
Kwa
asili utendi huu ni kiarabu iliyotungwa na al-Busiri inayoitwa Kasidatul’l
Hamziyyah fi ‘l-mada’ihi’ n Nabawiya yaani Kasida ya kumsifu Mtume Muhammad.
Katika Kiswahili utendi huu hujulikana kama Chuo cha Hamziyyah au Maulid ya
Hamziyyah au Hamziyyah tu.
Utungo
huu ni wa aina ya ukawafi amabao kiasilia ulikua na beti 456 na jumla ya mizani
15 kwa kila mshororo. Ambapo katika Kiswahili kuna beti 481, beti 8 za mwanzo
na 10 za mwisho zimeongezwa na mtarjumi wa kasida hii, Sharrif Aidarus.
Utenzi
huu ni maarufu sana katika ulimwengu wa fasihi, dini ya kiislamu na waswahili.
Umaarufu wake unatkana na kuimbwa kwake wakati wa sherehe za maulidi ya kumsifu
Mtume Muhammad kama ukumbusho wa kuzaliwa kwake kama asemavyo Lubis (1983)
alivyonukuliwa na Mutiso (2005:5) kwamba Hamziyyah kama kazi ya kisanaa
inakaribia kwa umashuhuri zaidi kuliko al-Burdah
Utendi
wa Hamziyyah umeitwa hivyo kutokana na kuishia kwake kwa abjadi ya kiarabu hamza katika mshororo wa mwisho yaani
kina cha mwisho cha utungo huo wa kiarabu. Fauka hiyo kuna maandishi yanayounasibisha
utungo huu na swahaba wa Mtume Hamza. Wanasema, “Hamziyyah ni dhehebu moja la
kiislamu lililoanzishwa na Hamzah bin Adrak. Yawezekana kwamba kasida hii ni
tunu kwa dhehebu hili. Yumkini utenzi huu uliitwa hivyo kwa kutaka kuusifu mji
mtakatifu wa Makka amabako hadi sasa kuna chuo kikuu kiitwacho Umm-al Qura kama
kasida yenyewe inavyoitwa. Yawezekana pia kasida hii iliitwa hivyo kwa sababu
ya kumkumbuka yule shujaa wa dini ya kiislamu aitwaye Hamza (Mutiso, 2005:5)
Kauli
hii haina ithibati. Kwanza hakuna dhehebu katika uislamu lililoanzishwa na
Hamza lijulikanalo kama Hamziyyah. Pia kuwepo kwa chuo kiitwacho Umm-al Qura
huko Makka sio sababu ya utenzi huu kuitwa hivyo bali ni sifa tu mtu apendayo
kutoa kwa kitu alichokithamini. Umm-al Qura maana yake ni “Mama wa Mji”.
Ukiliangalia jina na yale yaliyomo katika utendi hayana uhusiano. Hali
kadhalika dai la kwamba kasida hii inaimbwa kwa kumkumbuka shujaa wa kiislamu
Hamza ni uzushi kwani sifa zilizomo katika utendi huu ni za shujaa Muhammad na
si Hamza na hata anayetajwa ndani ya utendi ni Muhammad
Hivyo
utendi huu hauna maana nyingine zaidi ya kuwa ni utungo unaoishia na Hamza herufi mojawapo katika herufi za kiarabu. Na
hii haina maana zaidi ya kuwa herufi zilivyo herufi zingine za kirumi kama
a,e,i,o,u.
HISTORIA FUPI YA MTUNZI
Sharif
Muhammad bin Said Hammad Al- Bussir alikua ni mshairi wa Kimisri katika fasihi
ya kiislamu aliyeishi kwenye miaka ya 608-694 H (1212-1294 m). Kwa upande wa
elimu alijifunzia huko Cairo kwa Sheikh Dhahir. Alijifunza usufii, fasihi ya
kiislamu, kunga za lugha ya kiarabu, kukariri Quran Tukufu kwa Moyo, Historia
ya Uislamu, Hadithi na Sira ya Mtume Muhammad, kunukuu miswada, uchoraji na
utiaji wa nakshi
Kutokana
na kuwa na taaluma mbalimbali aliweza kutunga kazi nyingi sana, baadhi ya kazi
hizo ni utenzi wa Hamziyyah, Kasida ya
Burudai, Kasida ya Lamiyyah, Kasida ya Lahiyyah, Kasida ya Dariyyah, Kasida ya
Mimiyyah na Dhukr
HISTORIA FUPI YA MTARJUMI
Sharif
Sayyid Aidarusi bin Athmani, alikua ni mwanazuoni na miongoni mwa Maulana
mashuhuri wa karne ya 18 na 19 walioongoza katika usomi wa kidini na hata
kifasihi katika Afrika ya Mashariki. Alitafsiri kasida ya Hamziyyah kwa
Kiswahili cha Kingozi ambacho ni Kiswahili cha zamani sana kutoka katika Lugha
ya Kiarabu, Aidarus aliishi Pate nchini Kenya
TAREHE YA KUTARJUMIWA
UTENDI WA HAMZIYYAH
Ama
tarehe ya kutarjumiwa au kuandikwa kwa utendi huu kunahitilafiana miongoni mwa
wataalamu wa fasihi ya Kiswahili waliouhakiki japo wengi wao wanakubaliana kuwa
yawezekana ilitarjumiwa kabla ya mwaka 1652. Miongono mwao ni Knappert (1968,
1969, 1973, 1979, 1985), Hinchess (1936), Kijumwa (1934), Mutiso (2005),
Mulokozi na Sengo (1995). Kuna wanaosema kuwa ulitarjumiwa mwaka 1652 (1257 AH)
(Mulokozi 1996:144), pia 1749(1162, AH) (Mkele 1976) amabpo Hinches anasema
kuwa mpaka mwaka 1936 ulikuwa na miaka 144. Hivyo yawezekana kuwa utenzi huu
ulitarjumiwa kabla ya mwaka 1652. Tatizo la kutokujua tarehe sahihi ya
kuandikwa kwa utenzi inaweza kuwa ni asili yake ya usimulizi ambayo kuipata
tarehe sahihi kunahusishwa na kutokuwepo kwa kumbukumbu mbalimbali za
kihistoria zilizohifadhiwa katika jamii husika.
YALIYOANDIKWA KUHUSU
UTENDI WA HAMZIYYAH
Knappert
(1968) aliandika kuhusu utendi wa Hamziyyah katika mada yak eta “The Hamziyyah
Deciphered” na mwaka (1979) aliandika “The Oldest Islamic Poetry: The
Hamziyyah”. Naye Mkelle katika kiango (1976) aliandika “Hamziyyah-The Oldest
Swahili Translation” na Abdallah (haina tarehe) aliandika “Tanzu za Ushairi wa
Kiswahili na Maendeleo yake”. Ridhiwani alitafsiri Hamziyyah kwa Kiswahili
rahisi japo ilionekana ni tafsiri sisisi.
Vile
vile Hinches alinukuu beti 96 wakati Knappert (1968) alinukuu beti 60-70 na
kuzitarjumu kwa lugha ya kiingereza. Mkelle nae katika uchunguzi wake aliishia
njiani na hivyo Ridhiwan kuthibitisha kuwa kasida hii ngumu kutafsiri.
Hivyo
inasadikika kuwa kasida hii ya Hamziyah haikutafsiriwa kikamilifu kwa lugha
yoyote ya kimagharibi (Knappert 1968, Mutiso 2005)
MUHTASARI WA UTENDI
Utendi
wa Hamziyyah unasimulia kuhusu sira ya Mtume (S.A.W). Mwandishi ameonesha kuwa
Mtume (S.A.W) alizaliwa katika kabila bora kuliko zote za kiarabu na katika
ukoo wa Banni Hashim ambao ni kati ya koo za kwanza zilizo tukufu kwa
Makureshi.
Mtume
alipozaliwa matukio tofauti yalitokea mfano, kuanguka kwa jumba kubwa la
mikutano la Kisra la Mfalme wa Uajemi (Ufursi) lililoyumbayumba na kupasuka na
kuporomoka kabisa. Inasemekana pia siku hiyo Mahabushia waliazimia kuuteka mji
wa Makka baada ya kuwa Yamah yote imo chini ya mikono yao. Hivyo Mwenyezi Mungu
aliwaletea ndui, yakaangamia majeshi yao kwa muda mfupi na inasemekana
walipukutika kama kuku.
Vile
vile mito na chemichemi za Mafursi zilikauka. Jambo lililopelekea huzuni
majumbani mwao sababu ya kuzimika kwa mioto ya Mafursi ambayo walikuwa
wakiabudu nyumbani mwao kwa miaka mingi iliyopita. Usiku alipozaliwa mtume
(S.A.W) nyota zenye mianga zilikaribia chini alipokuwa na kuangaza eneo hilo na
pande zote za dunia. Mwangaza uliwawezesha wakazi wa Makka kuona jumba la
mfalme Kisra. Vyote vilivyomo Makka vikang’ara kutokana na nuru ya Muhammad
(S.A.W). hata waliokuwa Urumi wakaweza kuyaona makasri hayo ya Kaizari na
kuiona Makka vizuri
Wakati
alipozaliwa alikuwa ameangalia juu mbinguni, kasha alipiga chafya na kusema
“Alhamdulilah” nao malaika wakajibu “Mwenyezi Mungu akubariki”
Mama
yake akiwa na ujauzito wa miezi nane, baba yake akafariki. Kama ilivyo desturi
ya waarabu, wanawake (wazazi) hawanyonyeshi watoto wao bali hunyonyeshwa na
mama wengine. Wanyonyeshaji walimkataa mtume sababu alikua ni yatima na maskini
na kusema kuwa waingeweza kulipwa.
Hatmaye
akanyonyeshwa na Halima, mwanamke ambaye baadaye maisha yake yakabadilika na
kuwa mazuri zaidi kwani wanyama wake waliokuwa hawatoi maziwa wakaanza kutoa
maziwa kwa wingi wakati jamii nyingine hazikuwa na hata jani bichi la kulishia
wanyama.
Mtume
(S.A.W) alipofikisha miaka sita, akafiwa na mama yake, hivyo kulelewa na babu
yake bwana Abdul Mutalib.
Tangu
alipkuwa mtoto (mwenye kuanzia miaka miwili) malaika alikuwa akimpasua kifua na
kumshona ili kuhifadhi siri katika kifua chake. Alipasuliwa pia kutolewa
kipande cheusi cha nyama(damu) na kukisafisha. Siri alizowekewa alizuiliwa
asizitoe mpaka atakapoamriwa aeneze.
Tangu
utotoni mtume alizoea kwenda pangoni Hirrah ili kumwabudu Mwenyezi Mungu. Moyo
wake, miguu na viungo vyote vya mwili wake vilikuwa imara na dhati katika
kumwabudu Mwenyezi Mungu.
Mwenyezi
Mungu alipoamua kumtuma Mtume kuja duniani alituma vimondo kuilinda njia yake
kutokana na majini. Vimondo viliwafukuza majini kutoka pale walipokuwa
wakisikiliza habari za siri, kwani kuzaliwa kwake kulimaanisha mwisho wa nguvu
za Wahayi na Makuhani juu ya mambo ya Mbinguni.
Mtume
alipopewa utume vitu vyote visivyokuwa na roho kama vile miti na mawe viliweza
kumshuhudia na kumuunga mkono vikisema “Assalaam Aleikum”. Pia vitu hivyo
vilisema maneno fasaha ambayo Makureshi wasingeweza kuyasema.
Katika
hali ya utume alipaishwa mbinguni, mbingu ambayo hakuna mtume aliyewahi
kufikishwa. Jamii yake na wote waliomzunguka walimkana, aliumizwa, kusumbuliwa
na kudharauliwa zaidi kila alipowalingania katika kumcha Mwenyezi Mungu.
Japokuwa wote waliokuwa hawamwamini waliangamia, vitu vilivyomtii vilikua ni
pamoja na mijuzi na paa pia mtende aliokuwa anauegemea ulikua ukimtii hali
iliyopelekea kukimbiwa na watu waliogopa. Mtume aliposafiri kwenda katika
biashara zake Sham, baada ya kukosa kivuli na kuketi kwenye jua, wingu na mti
mkubwa vilimfunika.
Siku
moja baada ya mateso makubwa, Mwenyezi Mungu alimwamuru ahame mji wa Makka,
akaondoka na rafiki yake aitwae Abu-Bakr. Baada ya kujua kuwa walifuatwa
wakaingia katika pango amabapo njiwa wawili walitaga mayai katika mlango wa
pango na buibui alitandaza tando lake hali iliyopelekea maadui kutojua
walikoelekea. Baada ya hapo walitoka na kuelekea Madina, ambapo njiani watu
wengi walimpenda kutokana na tabia zake nzuri na miujiza aliyokuwa anaifanya,
mfano kuweza kumkamua mbuzi asiyekuwa na maziwa kutoa maziwa yaliyotosheleza
watu wote waliopo hadi kubakiza mengine.
Katika
utume wake alipigana vita tofauti na maadui wa Uislamu na kushinda japokuwa
nguvu jeshi lake halikuwa kubwa zaidi ya maadui. Mwisho watu kutoka mataifa
tofauti walimkubali na kuweza kusimamisha dola ya Kiislamu.
Mtume
katika ujana wake alimwoa bi Khadija, mwanamke aliyetambua tabia nzuri ya Mtume
(S.A.W) ya kumcha Mungu na kuzipa kisogo raha za dunia, baadaye alioa wake
wengine kumi hivyo kufikisha jumla ya wake kumi na moja.
UCHAMBUZI
WA UTENDI WA HAMZIYYAH
Finnegan
1970 alisema kuwa katika fasihi simulizi ya kiafrika hakuna tendi bali kuna
tendi andishi na sifo tu. Kauli hii ilitokana na vigezo alivyovitumia vya tendi
za kiyunami amabazo aliziita ni tendi halisi. Vigezo alivyotumia ni:
- Utendi
uwe katika umbo la ushairi na si katika nathari
- Utendi
uwe na urefu wa kutosha
- Uwe
ni utungo mmoja usiwe ni mkusanyiko wa tungo zinazohusisha visa mbalimbali
ambavyo pengine havina uhusiano ulio dhahiri.
- Uzungumzie
mambo yahusuyo shujaa na kusawiri matukio ya kiutendi kama kuzaliwa kwa
shujaa, masahibu yake, safari zake, uongozi wake kwa watu wake na kifo
chake.
Kauli
hii ilipingwa na wataalamu mbalimbali kama walivyoainishwa na Mulokozi
(2002:2), baadhi yao ni ; Biebuyk (1972;1976;1978), Johnson(1978;1980),
Mbele(1977), Okpewho (1976;1977;1979) na Mulokozi(1975;1980;1981;1983) ambao
walifanya utafiti wa kina na kuibua hoja zifuatazo:
Mbele
(1977) alikanusha usemi wa Finnegan kwa kutumia utendi wa Sundiata wa Afrika ya
Magharibi ambao unatetea umwinyi na kulitukuza tabaka la Mamwinyi. Kwa maoni
yake anaona kuwa utendi wa Sundiata unaingia katika sifa zilizotajwa
Okpewho
(1977) alitumia kipengele cha muundo ili kukanusha dai la Finnegan, alitumia
tendi za Mwindo na Kambili na kuzibainisha sifa za kimuundo, kisanaa na
kiutunzi za tenzi hizo ukilinganisha na sifa za tenzi za mataifa mengine na
kuhitimisha kuwa tungo hizo pia ni tendi. Miongoni mwa sifa hizo ni fomula,
topo, uhusiano, takriri, na malumbano ya wahusika.
Biebuyk
(1978) anamuunga mkono Mbele na Okpewho katika kuthibitisha kuwa Afrika kuna
tendi simulizi. Yeye anaona kuwa kauli ya Finnegan imetokana na ufinyu wa data
alizopata.
Mulokozi
(2002) ni miongoni mwa wataalamu waliothibitisha uwepo wa tendi simulizi barani
Afrika. Yeye alitumia utenzi wa Nanga ujulikanao kama Utendi wa Kachwenyanja ambao ni maarufu mkoani
Kagera, Tanzania. Alisema kuwa utenzi wa Kaachwenyanja na halisi si kwa mujibu
wa vigezo vya Finnegan tu, ambavyo havitoshelezi, bali pia kwa mujibu wa vigezo
vingine vya kiulimwengu, ambavyo huuchukulia utendi katika dhana ya umbo lake
la asili la utendaji na si katika maana finyu ya kuwa katika maandishi tu.
Ukiwachunguza
wataalamu wote hawa wanaipinga kauli ya Finnegan na kutetea kuwa tendi katika
Afrika zipo, tena zinaakisi mifumo mbalimbali katika jamii husika.
Makala
hii inalenga kutoa mchango katika mjadala huu, hivyo tutachambua utenzi wa
Hamziyyah kwa mujibu wa sifa za utendi alizozitaja Finnegan na vigezo vingine
vya kilimwengu na zile alizoziongezea Mulokozi(1996:86)
A: UMBO LA USHAIRI
Hiki
ni kigezo kimojawapo cha utendi ambacho Finnegan anakisisitiza. Dhana ya
ushairi aliyoikususudia hapa ni ile ya nudhumu(verse) na si ushairi. Nudhumu ni
utungo wowote wenye umbo la kishairi yaani wenye mpangilio wa maneno, urefu wa
mistari, beti, vina n.k hata kama utungo huo hauna uzito ule wa kishairi kama
matumizi ya lugha ya picha, sitiari, maudhui ya kishairi, hisi taswira n.k
Japo
yeye mwenyewe katika ukurasa wa 10 anakubali kuwa si lazima utendi mzima uwe
katika ushairi bali anakiri kuwa utungo mzima unaweza kuwa utendi.
Hivyo
kulingana na maelezo hayo tunaweza kuthibitisha kwa kuangalia kama kigezo hicho kinapatikana
katika utendi wa Hamziyyah kwa kuziangalia sifa pambanuzi za ushairi wa utendi
ambazo yawezekana Finnegan ndizo alizozikusudia japokuwa hakuzitaja
- Vina na
Mizani
Utendi
wa Hamziyyah una urari wa mizani na kina cha mwisho kinachofanana na utendi
mzima. Mizani ya utendi huu ni 15 kwa kila mshororo na kina chake ni ‘ma’ kwa
utendi wa Kiswahili na herufi Hamza katika utendi wa kiarabu kwa kila mstari wa
mwisho, Mfano ubeti wa 37
A li
zi wi li
ya ma mwi
sho ni hi
fa dhi ya
ke
Na ku te u
li wa ta
ngu mwa ndo
M tu mi
mwe ma
1 2
3 4 5
6 7 8
9 10 11
12 13 14
15
Hivyo
kama kigezo cha urari wa vina na mizani kitachukuliwa kama uthibitisho wa
utendi kisanaa basi Hamziyyah ni miongoni mwa tendi zilizomo Afrika. Ni beti
mbili (33 na 164) tu ambazo kina chake ni mwa,
yawezekana mwandishi hakutaka kuharibu sifa mojawapo ya Mtume yenye jina la
Tumwa.
- Lugha
Lugha
iliyotumika katika utendi huu ni ya Kiswahili kilichosheheni lahaja za
Kiswahili na msamiati wa kiarabu. Lugha Y Kiswahili iliyotumika ni ngumu yenye
kutumia maneno ya Kiswahili cha kale; Mfano, matumizi ya e/ili yanayowakilisha
wakati uliopita; mfano ingile-aliingia, jiile-alikuja, nsomeele-nilisoma,
weene-aliona. Hizi zinatuonesha mabadiliko mbalimbali ya kiisimu. Vile vile
lugha hii inaonesha uhusiano na lugha nyingine za jamii mbalimbali za Tanzania,
mfano katika ubeti wa 130 kuna neno kanwa, katika jamii nyingi za kibantu kanwa
ni mdomo
Pia
lahaja zilizopo ni za Chimwini, Kitikuu, Kipate, na Kiamu; Maneno yaliyotumika
kutoka lahaja hizo ni kama; kwechu—kwetu, fungula—fungua, lokota—okota,
mkila—mkia, tala—taa, tukula—chukua. Matumizi mengine ya lugha yaliyojitokeza
ni kama:
- Lugha ya
Picha
Hii
ni mbinu ya kishairi inayotumika kuunda taswira mbalimbali juu ya kitu
kinachozungumzwa katika mawazo ya msomaji/msikilizaji. Mara nyingi hizi hugusa
vionjo vya msikilizaji au msomaji kama kuona, kusikia, kuhisi, kuonja na
kugusa. Hivi vyote huungana na kuleta taswira ya kile kinachokusudiwa. Taswira hizo
zaweza kuwa za kimaelezo au za kiishara. Ntingi ya taswira(picha) zilizomo
katika utendi wa Hamziyyah ni zile za miujiza iliyotokea katika maisha ya Mtume
Muhammad (S.A.W). miongoni mwa taswira (picha) hizo ni:
Ubeti
wa 23-28 wakati wa kuzaliwa kwake kukiambatana na Falme na majumba kuanguka,
kichwa kuelekea juu hii inaonesha ishara za kuwa daraja la juu. Katika ubeti wa
66-68 alivyojihifadhi katika pango huku akilindwa na Njiwa, Kanga na Buibui
inaonesha upekee wake unaopelekea kuhifadhiwa na Mwenyezi Mungu pia ubeti wa
128 taswira ya upole wake wa kuweza kuvumilia kashfa, huonesha utakazo aliopewa
na M/Mungu wa kuwa mvumilivu. Taswira zingine nyingi zimeambatana na sifa zake
na vitimbwi alivyofanyiwa na maadui zake waliomkataa, mfano kumpiga mawe, kumtilia
sumu na zinginezo zinazopatikana katika beti za; 28-36b, 37-43, 46-48, 53-56,
73-79, 106, 108, 113-115, 157-163 na 269-274.
- Sitiari
Ni
tamadhali ya usemi ambayo kwayo kitu, matendo ya kitu au vitu vyenye tabia
inayofanana hulinganishwa. Au ni pale kitu kimoja kinapopewa sifa na kuchukua
nafasi ya kitu kingine kisichohusiana nacho. Katika ulinganisho wa vitu mtunzi
hatumii vilinganishi kama vile; kama, kama vile, n.k. katika utendi wa
Hamziyyah sitiari zinajitokeza katika ubeti wa 4,10,11,81,105,127,128,140,142,215,266
n.k Mfano katika ubeti wa 4
Uwe ndiwe Tala
ya fadhila na mayonjia
Nuru
hazinawiri pasipo nuru yako njema
Maana
yake ni wewe ni taa ya kila tendo bora na ndio asili ya nuru zote, ndio asili
ya yote yalito mema na yenye uongofu. Sitiari hii na zingine zilizotumika
huonesha sifa ya Mtume zilivyomiminika kwa Waislamu na kumtukuza kuwa ni
kiongozi wa kila jema.
- Tashbiha
Ni
tamathali ya semi ambapo kitu, vitu, hali moja au mbili na zaidi hulinganishwa
na kitu kingine kwa kutumia viunganishi vilinganishi kama; ja, mithili (ya),
mfano (wa), kama, fanana na....., vile vile, sawasawa na......, n.k. Kufanana
huku mara nyingi huwa ni ushahibiano wa hali ya utendaji au maumbile kama vile sura,
umbo, nguvu, n.k . katika utendi wa Hamziyyah zipo tashbiha kadhaa baadhi yake
zinapatikana katika ubeti wa 3,12,108,112,159,267,306-309,318-320, n. K Kwa
mfano ubeti wa 11
Napendezwa tena na uso wako ingawa Jua
Maana
yake ni: Napendezwa na uso wako ulio kama jua. Usemi huu huitabanisha hadhira
ubora wa Mtume (S.A.W) kwa yale ayadhihirishayo, kwamba huwatoa watu katika
ujinga.
- Tashihsi
(Uhusishaji)
Mbinu
hii ni ile ya kukifanya kitu kiwe na maumbile/tabia ya nafsi ya mwanadamu.
Katika mbinu hii hali na vitu visivyo na uhai hupewa sifa na hisia za binadamu.
Kama vile wadudu, miti,ndege, na wanyama. Wakati mwingine vitu hivi huongea na
kutenda kama binadamu. Hali hii inajitokeza katika utenzi huu, mfano:
- Vitu
visivyo hai kumsalimia na kumsujudu Mtume Muhammad (ubeti 46-47)
- Wanyama
kuwa na akili hata zaidi ya Wanadamu mfano ndovu kukataa kuiharibu
al-ka’ba (ubeti wa 61-63)
- Changarawe
na mawe viliswali na kumuunga mkono Mtume Muhammad (ubeti wa 63)
- Mijusi
kusema (ubeti wa 65)
- Panga
kukataa kumuua Mtume (ubeti wa 108)
- Nyama
ya sumu kusema kuwa imetiwa sumu (ubeti wa 116-117)
- Wingu
kumkinga (ubeti wa 138)
- Mlima
kutetemeka kwa furaha (ubeti wa 156,183) na zingine kama
168,291,283,284,285-286,322-323 na 453. Tashihsi hizi na zingine
huthibitisha miujiza iliyotokea katika maisha ya Mtume (S.A.W) ambayo
iliaminika kuwa ujio wake ni tishio kwa kila kitu au kiumbe.
- Taashira/Ishara
Kuna
matumizi makubwa ya mbinu hii. Taashira ni neno, kitu au tukio linaloficha
maana au hisia. Ishara hutumiwa kuwakilisha kitu ambacho hatungetaka kukitaja
moja kwa moja. Miongoni mwazo ni:
- Ishara
za wakati wa kuzaliwa Mtume Muhamad zinatuonesha upekee wa mtume Muhammad
kama shujaa anayezaliwa tofauti na mitume wengine (ubeti wa 15)
- Hii
ni ishara ya ushindi wa uislamu duniani kote. Mito na chemchem za Mafursi
zilikauka kuonesha ushindi wa uislamu juu ya dini nyingine duniani (ubeti
wa 17)
- Kuzaliwa
Muhammad kichwa kimeelekea juu ni ishara kwamba atapandishwa daraja la
kifalme (ubeti wa 24-25)
- Ishara
ya kutolewa kipande cha nyama nyeusi (ubeti wa 41) ni taashira ya kutolewa
nyongo kifuani mwake ili aondokane na hasira pindi awalinganiapo watu
wake. Ishara hii ni alama ya kutakaswa kwa Mtume Muhammad.
- Mutwazi/ukaya
(ubeti wa 54) ni ishara la vazi takatifu ambalo mwanamke wa kiislamu
aliloruhusiwa kulivaa.
- Matumizi ya
Semi
- Kuipa
nyongo dunia ikiwa na maana ya kuachana na mambo ya dunia na kuwa waumini
thabiti (ubeti wa 34)
- Kupewa
mkono mweupe yenye maana ya kutakiwa heri na Mtume Muhammad(ubeti wa 366)
- Njia
nyeupe ni njia nyoofu isiyokuwa na shaka, shida au hatari yoyote
- Matumizi ya
Balagha/Tashtiti
Hii
ni mbinu ya kuuliza maswali ambayo majibu yake mtunzi anayafahamu, lengo huwa
ni kusisitiza ujumbe anaotaka kuufikisha kwa aliowakusudia. Nia ya mtunzi huwa
ni kufahamu zaidi wazo husika na vile vile kutoa msimamo wake pamoja na
kumtazamisha msomaji. Mara nyingi maswali haya lengo lake ni kuamsha ari ya
msomaji na kumfanya atafakari zaidi juu ya kinachozungumzwa. Mtunzi kupitia
balagha huwachochea wasomaji wake ili wawaze kufikiria zaidi juu ya jambo
analolielezea, baadhi ya maswali ya balagha yanapatikana katika beti zifuatazo:
- Ubeti
wa 1, 20, 102, 106 na 108 zinaonesha uwezo wa shujaa Muhammad dhidi ya
maadui zake. Lengo la maswali haya ni kuwakejeli maadui na wapinzani wa
Mtume Muhammad na kuonesha kuwa wasingeweza kumdhuru kwa sababu alikuwa na
uwezo kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
- Pia
ubeti wa 200-268 ametumia balagha kuonyesha tofauti baina ya Manasara,
Mayahudi na Waislamu. Mtunzi amewaonesha wasomaji kwa kulinganisha makundi
hayo matatu lengo likiwa ni kuzibeba dini za Manasara na Mayahudi na
kuonesha kuwa dini ya uislamu ndiyo inayopaswa kufuatwa ulimwenguni kote.
Ameonesha namna ambayo manasara na mayahudi wasivyoweza kutii na kufuata
yaliyomo katika vitabu vyao vay Taurati n biblia (Injili)
- Kejeli
Ni
mbinu ambayo mtunzi anaitumia ili kumtweza au kumdunisha mtu kwa kupewa sifa
ambazo hazimstahili. Mara nyingi maneno yatumiwayo huwa ni ya kuumiza, kuchoma,
kukatisha tama na kutia uchungu. Mbinu hii imetumika sana hasa pale mwandishi
alipozikejeli dini za Ukristo na Uyahudi kwani kwa maoni yake Uislamu ndio dini
bora na inapaswa kufuatwa na watu wote na kuwahimiza Waislamu wabakie katika
Uislamu. Mfani ni katika ubeti wa 218 mwandishi anasema;
Enyi wenye Zuo tuyuzeni kula zilipo
Kuthalithi
au kudhihiri walo wa nyuma
Maana
ya kejeli hii ni kwamba enyi msio amini tuelezeni sababu za kuwa na utatu au
kudhibitika kwake kwa waliotangulia? Kejeli hii imetumika kama changamoto ya
kutathmini kila unachoamua kukifuata.
Na
ubeti wa 231;
Mwamba
liwuwiwa ni Yahudi mzumuwo
Wali na fufuo wenu kwayo dawamu?
Maana
yake ni kuwa wasema aliuliwa na Mayahudi. Hii inaonyesha kuwa mwandishi
amekusudia kuwafahamisha wanaoamini kuwa Yesu aliuliwa, kwamba Mayahudi
waliwekewe mtu mfano wa Yesu na wakamuua hali ya kuwa Yesu alipaishwa mbinguni.
- Majina ya
Lakabu
Lakabu
ni neno la kiarabu lakab lenye maana
ya sifa ajipayo au apewayo mtu kutokana na tabia Fulani aliyonayo ya kipekee.
Ni jina la sifa ya kubandikwa apewayo mtu au mhusika kwa sababu ya tabia Fulani
ya kipekee (uwezo wa kuwa na sifa ya kitu kingine) Mfano:
- Mtume
Muhammad ana majina ya kalabu chungu nzima, Abdul Qarim, Buhari,Tumwa, Mtume, Jua, Kifungo, Kifunuo, Mjuzi,
Kipenzi/Mpenzi, Mtengwa, Muharamu, Mustafa, Muungwana, Mwema, Mwongozi,
Nuru, Nyota ya Jaha, Sayyid, Taa.
Majina yote haya yanabshiria tabia njema za Mtume Muhammad.
- Abu
Jahli maana yake ni baba wa wajinga (ubeti wa 109)
- Ritifaa
Hii
ni mbinu ambayo mshairi huonyesha kuwa anaongea na kuhutubia mtu au kitu
ambacho hakipo. Katika mbinu hii kitu kisicho na uhai kusifiwa na kusimuliwa
kama kipo. Mbinu hii imetumika sana katika kasida hii. Mtunzi anazungumza na
kuhutubia maswala yamuhusuyo Mtume Muhammad, familia yake, mswahaba (Makhalifa)
na walioahidiwa kuingia peponi baada ya kufa ingawa watu hawa wote tayari
wameshafariki. (ubeti wa 355-447). Hii ni kutaka kuthibitisha kuwa Mtume
Muhammad alikuwa shujaa. Mfano ubeti 433;
We una umati mbawo kwamba
watamaniye
Kwawe ambia upewepo sawu
umama
- Chuku
Mbinu
hii imetumiwa kwa kiasi kikubwa katika kasida hii ya Hamziyyah. Kutia chuku ni
kukuza jambo Fulani kupita kiasi au kutia tungo chumvi. Matumizi ya mbinu hii
si kwamba mtunzi huwa na nia mbaya, bali anakuwa na lengo la kusisituza ujumbe
unaowasilishwa na kukamilisha sifa za shujaa. Mbinu hii imetumika sana katika
utendi huu wa Hamziyyah, mfano:
- Katika
sifa za mtume si za kawaida kuwa kwa mwanadamu kama alivyokuwa yeye. Mfano
wa ubeti 127
- Katika
baadhi ya miujiza yake.
- Na
sifa nyingine zilizomkweza tofauti na uhalisia wake ambazo ni sifa za
Mwenyezi Mungu. Mfano ubeti wa 336-337 Mtume alimponya Ali hata kuona
kuliko mwewe.
- Mtume
kuzaliwa kichwa kikielekea juu.
- Takriri/urudiaji
Mbinu
hii husisitiza ama hushadadia ujumbe unaohusika ili msomaji apate athari ya
msisitizo huo. Kwa mfano mapigo ya muziki katika ushairi. Mtunzi hutumia mbinu
hii kwa lengo la kusisitiza jambo Fulani. Mfano katika ubeti wa 151;
Na kula shurutiwa sharutiwe jazaa kwima;
Pia
neno thama limejitokeza mara nyingi
katika beti mbalimbali, mfano ubeti 26 na 30.
- Mazida
Ni
mbinu ya urefushaji wa maneno ili kuleta urari wa mizani katika mshoshoro.
Mtunzi wa mashairi hufanya hivyo kwa nia ya kusawazisha mizani ya mishororo
yote katika ubeti 214, 221,263,271,274,339 kwa mfano ubeti 274 neno kulolani badala ya kulola; ubeti 271 neno mipotofu
badala ya potofu.
- Inkisari
Hii
ni mbinu ya ufupishaji wa maneno ambayo mtunzi huitumia kwa lengo la kuleta
urari wa mizani katika mshororo. Hapa silabi au mizani katika neno hufupishwa.
Katika utenzi huu kuna matumizi makubwa ya mbinu hii, aghalabu utenzi mzima
umesheni mbinu hii. Mfano ubeti 21: neno
apokeo badala ya alipopata ubeti
wa 24 neno atukule badala ya alichukua.
- Tabdila
Ni
mbinu katika ushairi ambayo mshairi hubadilisha sauti Fulani katika neno ili
kuleta uwiano Fulani, hususani mwishoni mwa kipande cha mshororo. Lengo ni
kupata kina kifaacho. Mfano ubeti wa 5, 30, 41, 42, 200 na 216. Katika ubeti 5;
neno Adama kutoka neno Adam, ubeti 42; neno dama kutoka neno damu.
Mbinu
nyingine ni:
- Fomula na
Topo:
Fomula
ni kigezo cha usimulizi wa tungo yoyote. Utendi simulizi hutungwa papo kwa hapo
mtunzi anaimba kwa kutumia vipande vya sentensi vilivyomo katika jadi ya
ushairi huo ambao huitwa fomula huku akipanga upya mawazo na matukio ya kijadi
yaitwayo topos. Hivyo haimpasi mtunzi kukariri maneno ya utenzi wote, bali
hujifunza tu fomula na topo za jadi zilizomo katika hazina ya fasihi ya jamii
yake na kuzitumia kutunga utenzi wake wakati akiteza. Hii hupelekea hadi mtendi
akaimba hata zaidi ya maneno 10,000 kwa mfululizo bila kuishiwa au kusahau.
Hii
inaashiria kuwa msingi wake ni kanuni ya kurudiarudia vina mizani na usambamba.
Katika kasida hii pia tumeona huo urudiajirudiaji mkubwa wa fomula na topo.
Mfano sifa zinazorudiwarudiwa za Mtume Muhammad. Hali kadhalika topo kadhaa au
vituko vina marudiorudio, kwa mfano
Ø Usambamba
Ni
mbinu ya kurudiarudia na kuambatanisha mistari, vipande vya mstari au sentensi
zenye kufanana au kukinzana kimuundo au kimaana, mtunzi hutumia dhana mbili
ambazo zinakinzana kimaana, lengo kuu ni kusisitiza ujumbe. Katika utendi huu
mbinu hii imetumika sana, mfano kuna usambamba wa kimaana,kidhamira,kiusawe na
kisintaksia.
Mathalani
katika ubeti wa 1 katika utangulizi kuna usambamba wa kimaana wa majina ya
Mwenyezi Mungu: ar-Rahaman na ar-Rahima
Naanza kwa jinale Bismillahi lenye adhama
Na ar-Rahamani Muwawazi na ar-Rahima
(Maana yake ni kuwa M/Mungu
mwingi wa rehema mwenye kurehemu)
Usambamba
mwingine ni wa kimuundo unapatikana katika beti zifuatazo:
- 154 Likabubujisha vula kuu siku sabaa
Wingu shushizalo pambiloza waliko ama
- 155 Kalomba iwingu ikandoka kisa kulomba
Na pa wenye nyocha
papishapo ziriba thama
- 156 Na watu wakaja kushitaki shida ya
wingu
Na mivula kuu shida
lake laudhi anama
- 157 Kalomba iwingu ikandoka kisa
kulomba
Vula ya kulomba
kunukakwe swifu alima
- 158 Vula kakasati ikakata mato kutola
Zitongoji zote na
kabila fufiwa vyema
Usambamba
huu unawez kutupatia kisa au ngano inayoweza kusimuliza hivi:
“Paliondokea mwarabu mmoja katika mji wa
Madina aliyemwomba Mtume(S.A.W) aombe kwa ajili ya kupata mvua katika mji huo
wa Madina ambao ulikumbwa na ukame kwa muda mrefu. Mtume aliomba sana na sala
yake ikajibiwa na Mwenyezi Mungu. Mvua kubwa ilinyesha kwa muda wa siku saba,
kama ilivyo tabia ya mwanadamu ya kutokuridhika wakaona mvua ile inawakera sana
hivyo basi Mtume Muhammad akaomba tena mvua ikaisha. Baada ya mvua kuisha nchi
yote na vitongoji vyake vikawa vinavutia kwa madhari nzuri ya chanikiwiti na
uhai ukarejea tena, wakaishi kwa raha mustarehe.”
B: KIGEZO CHA UREFU
Hiki
ni miongoni mwa vigezo alivyovitumia Finnegan kupambanua tendi. Anasema utendi
ni lazima uwe na urefu lakini hajasema kiwango hicho cha urefu ama kuwe na beti
kiasi gani na idadi ya mistari katika utendi mzima. Kwa kutumia kigezo hiki,
tunaona kuwa utendi wa Hamziyyah una urefu wa kutosha kwani una beti 449.
C: KISA
Finnegan
anasema utendi lazima uwe ni utungo mmoja. Usiwe ni mkusanyiko wa tungo unohusu
visa mbalimbali ambavyo yawezekana havihusiani. Katika utendi huu kisa
kinachosimuliwa ni cha Mtume Muhammad kuanzia kuzaliwa kwake, utoto wake,
kupewa utume, harakati za kueneza uislamu hadi kifo chake. Kwa maana hiyo basi,
ni kisa kinachojitosheleza na matukio yake yote yanawiana.
D: KUHUSU SHUJAA
Utendi
wa Hamziyyah unatimiza kigezo hiki sababu kisa kinachosimuliwa kinahusu
kuzaliwa shujaa Mtume Muhammad. Kuzaliwa kwake kuliambatana na miujiza mingi
mfano ubeti wa 13-18 na 58-61. Tunaoneshwa masahibu aliyokumbana nayo katika
kueneza uislamu Makka mfano ubeti wa 82-96 na 104-119. Halikadhalika
tunaoneshwa safari zake za kwenda Israa na Miraji: mfano ubeti 75-81, kutoka
Makka kwenda Madina ubeti 68-74. Vile vile tunaoneshwa uongozi wake ulivyokuwa
mfano ubeti wa 58-61. Hatimaye tunaoneshwa kifo chake.
Kutokana
na vidokezo hivyo ni wazi kuwa yaliyomo katika utendi huu ni mambo yanayomuhusu
shujaa Muhammad. Hivyo utendi huu umekidhi kigezo cha Finnegan kwamba utendi
ueleze mambo yanayohusu shujaa.
Ruwaza ya Shujaa
Shujaa
wa utendi huu ni Mtume Muhammad ambaye anaingia katika ruwaza ya shujaa ya
Campbell ya mwaka 1956, ambapo shujaa wa utendi huu anakuwa na sifa zifuatazo;
- Shujaa
ni wa tabaka la juu
- Kuzaliwa
kwa shujaa kunaambatana na matatizo na misukisuko kwa mfano ubeti 12-17.
- Kuzaliwa
kwake inakua ni tishio kwa jamii iliyokuwepo kabla ya kuzaliwa kwake.
- Shujaa
ananyonyeshwa na mwanamke wa hali ya chini mfano katika ubeti wa 32-33
- Shujaa
anakuwa na kuwatafuta wazazi wake.
- Shujaa
anaanza harakati za kutetea dini y a Uislamu.
- Mwishoni
anafanikiwa na kushika nafasi ya juu, mfano beti 252-281
Fomula ya Bowra ya e=m+ms
(U=V+M)
Fomula
hii nayo imejitokeza katika utendi huu
U=utendi,
vigezo vyote vya kiutendi vimejitokeza katika utendi huu
M=muziki,
utendi wenyewe unaimbika moja kwa moja kwani ni kasida.
V=vita,
masuala ya vita yamezungumzwa katika kutetea dini ya Uislamu mfano ubeti
262-276 Mtume ameonekana akipigana vita vya Badri na Hunaini.
Fomula simulizi
Pia
hii imejitokeza katika utendi huu. Hii ni kuthibitisha kuwa utendi huu
umetokana na usimulizi, unaanza kwa dua ya ufunguzi na kufunga kwa dua. Pia
urudiaji rudiaji wa maneno kama tulivyoonyesha katika takriri ni uthibitisho
kuwa ni utendi uliotokana na simulizi.
Kwa
kuwa utendi huu ni utendi wa Kiswahili shujaa wa utendi huu anafuata sifa za
shujaa wa waswahili ambazo ni:
- Shujaa
anatoka tabaka la juu
- Ni
jasiri
- Ana
uwongofu ‘baraka’
- Ana
jaala ya Mwenyezi Mungu
- Anapata
msaada wa Allah
- Anaungwa
mkono na watu
Kwa
mtazamo wetu tumeona kwamba sifa ya sihiri na udhaifu wa shujaa havijajitokeza
katika utendi huu.
Utendi na historia
Halikadhalika
utendi wa Hamziyyah unaweza kuwa wa kihistoria kwa sababu ya kumuelezea Mtume
Muhammad na kuasisiwa kwa dini ya
kiislamu ambaye anasadikika kihistoria alipata kuishi.
Utendi na utaifa
Vile
vile unaweza kuwa ni utendi wa utaifa kwa sababu maudhui mengi katika utendi
huu yamejikita katika kuelezea kanuni, mila na desturi za kuanzishwa kwa dola
ya kiislamu huko Makka na Madina.
Dini na kiyama
Pia
utendi huu wa Hamziyyah unahusu maswala ya dini na kiama mfano safari ya Mtume
Muhammad kwenda Miraji (Mbinguni) na watu walioahidiwa kuingia peponi
yanadhihirisha athari ya dini ya waislamu katika utendi huu.
Kuchanganya Tanzu
Tumeona
katika utenzi huu mwandishi amechanganya tanzu mbali mbali. Kuna hadithi na
baadhi ya aya za kurani alizotumia katika utendi huu. Mfano:
- Kisa
cha Isra na Miraji katika ubeti wa 68 -74 kimechukuliwa katika kurani
tukufu 17:1, 2:144, 149, 150, 191 na 217.
- Vita
vya Badri na Hunaini vinapatikana katika kurani tukufu sura ya 26:18,
30-31, 63 na 40:33
- Kupasuliwa
kwa kifua na moyo sura ya 50: 14
Pia
utendi huu ni wa kisira unatoa wasifu wa mtume tangu kuzaliwa kwake, misukosuko
aliyoipata hadi kifo chake.
Muktadha
wa utendi huu ni kati ya mwaka 1500-1750 BK kilikua ni kipindi cha misuko suko
ya mapambano kati ya wenyeji(waislamu) na wavamizi wa kireno (wakristo). Hivyo
utendi huu ulilenga kuhamasisha jamii ya waswahili kupambana na uvamizi wa
kireno ambao ulisadikika kumiliki misingi ya uzalishaji mali.
MAUDHUI
Kwa
ujumla maudhui yanayopatikana katika utenzi huu ni haya yafuatayo:
Falsafa ya maisha-
Maisha ni mapambano, sifa za mtume Muhammad kabla hajazaliwa, baada ya kuzaliwa
na misuko suko aliyoipata hadi kufa kwake ni dhahiri kuwa maisha ndivyo yalivyo
hasa kwa mashujaa wengi.
Utetezi na ufafanuzi wa
dini ya kiislamu- Dini ya kiislamu
imeelezwa kwa kiasi kikubwa katika utenzi huu. Mtunzi amelibainisha hilo kwa
kumsawiri shujaa Muhammad akipambana na wote waliokuwa wakiipinga na kwenda
kinyume na dini ya kiislamu mfano Manasara na Mayahudi waliokuwa na dhana
potofu ya utatu katika umoja. Kwa hiyo utendi umeonyesha dharau kwa dini hizo
na kuwahimiza waislamu wabakie katika uislamu wao. Ndio maana kulikuwa na
mapambano ya mtume dhidi ya maadui zake, shida na mateso vilitokea na baadae
uislamu ulishinda.
Pia
utenzi huu unatuonyesha imani kubwa katika dini ya kiislamu kutokana na miujiza
mbali mbali aliyokuwa anaionyesha Mtume Muhammad. Miujiza mingine ilihusisha
uwezo wa wanyama kuwa na akili na kusema na kutenda zaidi ya binadamu mfano
ndovu, ngamia, mijusi. Kwa kawaida wanyama kama hawa hutumika katika utendi ili
kumjenga shujaa.
Matumizi ya namba
Katika
utendi huu kuna matumizi ya namba tano na namba saba, mfano;
- Maadui
watano wa mfalme waliokufa kutokana na maradhi yasiyotibika ubeti wa 88-94
- Waislamu
wema watano ubeti wa 95-99
- Mvua
kubwa ilinyesha kwa muda wa siku saba ubeti wa 154-159
Namba
hizi kwa jamii ya waswahili zina maana, namba tano ina maana ya swala tano
zinazotekelezwa na waislamu kila siku na namba saba maana yake ni mbingu saba.
Aidha
kuna kufanana kwa maudhui ya utendi huu na tendi nyingine au vitabu vingine
mfano;
- Kurani
tukufu
- Tendi
zilizoandikwa zenye maudhui kama hayo ni pamoja na Utenzi wa Tambuka,
Siri’I asilali, Ras’I Ghul na Inkishafi.
- Vile
vile utendi huu umepelekea kuibuka kwa utendi nyingine kimaudhui na kifani
mfano Utenzi wa Inkishafi.
MOTIFU
Hiki
ni kipengele kingine kinachojitokeza katika utendi huu. Motifu ni kipengele cha
kifani na kimaudhui kinachojirudia rudia tungo mbali mbali. Motifu zilizojitokeza
katika utendi huu ni hizi zifuatazo;
Motifu ya kuteseka kwa
mitume na manabii. Motifu hii inaonekana
kujitokeza sana kwa mitume katika harakati za kueneza dini, mfano Muhammad
katika utendi huu ameteswa, amepigwa, na hata kupingwa na makureshi wakati wa
kueneza dini ya kiislamu. Hali hii imeendana na mateso waliyoyapata Manabii na
Mitume wengine katika historia kama Mussa, Yesu (Issa), Nuhu na wengineo.
Motifu ya watoto
kunyonyeshwa na wazazi wasio wao. Katika utendi huu
shujaa Muhammad amenyonyeshwa na Bi Halima mwanamke wa shamba, kwa waarabu hii
ilikua ndiyo desturi yao lakini kiutendi hali hii huijenga ruwaza ya shujaa.
Motifu ya safari. Hii
ni motifu nyingine inayojitokeza katika utenzi huu. Muhammad anasafiri kwanza
kutoka Makka kwenda Yerusalem na Mbinguni. Pili anasafiri kutoka Makka kwenda
Madina.
Motifu ya ukarimu yaani
shujaa kupewa mali au nyumba. Katika utendi huu Muhammad anakirimiwa na
waislamu wa Madina pindi alipohama kutoka Makka kwenda Madina kama
ilivyojitokeza katika tendi za Ras’IGhul na Nyakiiru Kibi.
Motifu ya ukatili wa
wanawake waliokataa kumnyonyesha mtume, mwanamke
mbeba kuni na mwanamke aliyeweka sumu katika nyama ya mtume.
Motifu ya mtoto wa ajabu.
Nayo inajitokeza katika utendi huu.
Miujiza iliyojitokeza kabla na baada ya kuzaliwa kwake inadhihirisha ushujaa wa
Muhammad kutokana na uajabu alioambatana nao.
Mchango wa Wanawake
katika kumjenga shujaa wa utendi;
- Amina
huyu ni mama yake ambaye (siku za uhai wake) alikuwa naye sambamba tangu
kuzaliwa.
- Khadija
na wake wenza walimpa moyo na kumliwaza dhidi ya maswahiba aliyokuwa
akiyapata, pia walikuwa tayari kuvumilia ugumu wa maisha aliokumbana nao
shujaa Muhammad (S.A.W)
- Wengine
ni Zainab Bint Ali-Harith beti 116-117, Umm Ma Abad beti 167 na Ummy Jamil
ubeti 113-115.
Kwa
kuhitimisha tunaweza kusema kwamba utenzi wa hamziyyah licha ya kutoa maadili
ya dini ya kiislamu una mchango mkubwa katika ushairi wa Kiswahili kwani ni
mojawapo ya utenzi wa awali unaohusu matukio ya Uarabuni na Mashariki ya Kati
wakati wa kuasisiwa kwa uislamu na ni miongoni mwa kazi za mwanzo
zilizotafsiriwa katika lugha ya Kiswahili, pia uthibitisho kuwa Afrika ina
tendi toka zamani na ni hifadhi ya lugha ya kale. Vile vileumepelekea
kupatikana kwa bahari ya Hamziyyah katika ushairi na hivyo kuonesha uhusiano wa
ukaribu uliokuwepi kati ya Afrika Mashariki na Afrika ya Kaskazini.
MAREJELEO
Finnegan,
R (1970). Oral Literature in Africa.
The Clarendon Press. Oxford.
Mkelle,
M.B (1976). “Hamziyya, the oldest Swahili Translation,” Kiswahili Vol.A6/1, kur
71-75.
Mulokozi
M.M (1989). ‘Tanzu za Fasihi Simulizi’ katika Mulika na. 21, Dar es Salaam.
TUKI
Mulokozi,
M. M. na T S Y Sengo (1995). History of
Kiswahili Poetry: A.D 1000-2000.
I.K.R, University of
Dar es Salaam.
Mulokozi,
M.M (1996) Fasihi ya Kiswahili. Chuo
Kikuu Huria Cha Tanzania.
Mulokozi,
M.M (2002) The African Epic
Contoversy:Historical, Philosophical and Aesthetic
Persipectives on Epic Poetry and Performance,
Dar es Salaam. Mkuki na
Nyota Publishers.
Mutiso,
K (2005). Utenzi wa Hamziyya. Dar es
Salaam: TUKI
Sengo,T.S.Y
(1976). Shabaan Robert: Uhakiki na
Maandishi yake. Longman, Dar es Salaam.
Wamitila,
K.W (2003) Kamusi ya Fasihi:Istilahi na
Nadharia. Nairobi: Focus Publications
Ltd.
No comments:
Post a Comment
syliverymanyama@gmail.com