Flower
Flower

Wednesday, January 29, 2020

Utendi wa Rukiza



Wataalamu mbalimbali wametoa maana ya utendi katika mitizamo tofauti tofauti ,miongoni mwa watalaamu hao ni kama wafuatao;
Mulokozi (1996:85) utendi ni utanzu mashuhuri sana katika kundi la ghani-masimulizi. Utendi ni ushairi wa matendo. Ni utungo mrefu wenye kusimulia matukio ya kishujaa yenye uzito wa kijamii au kitaifa. Matukio haya huweza kuwa ya kihistoria na visakale/ visasili.

Wamitila (2003:333) anaelezea utendi kuwa ni shairi refu la kisimulizi linalozungumzia kwa mapana na mtindo wa hali ya juu matendo ya mashujaaa au shujaa mmoja. Kimsingi utendi huwa na sifa nyingi na huweza kuleta pamoja hadithi ya kishujaa, mugani, visasili, historia pamoja na ndoto za taifa fulani. Anaendelea kusema kwamba kuna aina mbili za tendi ambazo ni tendi zinazohusisha fasihi simulizi na utendi wa kifasihi/ andishi.

Sifa za utendi wa Kiafrika    
Ruth Finnegan alifanya utafiti juu ya tendi za Kiafrika akagundua kwamba Afrika hakuna tendi bali kuna sifo. Katika kitabu chake kilichoandikwa mwaka 1970 anaeleza kuwa utanzu wa utendi hautokei sana Afrika. Katika kuelezea sifa za utendi , Finnegan alibainisha sifa nne za tendi simulizi ambazo ni nudhumu, urefu yaani utendi lazima uwe mrefu, sifa ya upatanifu yaani utendi ni utungo wenye visa vilivyounganika kimantiki na maudhui ambayo yanapaswa kusimulia maisha na matendo ya kishujaa. KARATASINI 
 Wataalam wengine waliona sifa alizotoa Finegan hazijajitoshereza na hivyo wakaongeza sifa nyingine za utendi,wataalamu hao ni Okpewho (1979), Jonhson (1986) Mulokozi (1987)  wamethibitisha kuwa utendi ni fani iliyoonea sana Afrika na wameongeza sifa za utendi. Sifa hizo ni kama zifuatazo: Utendi lazima uwe ni masimulizi, hutolewa kishairi, huhusu matukio muhimu ya kihistoria au kijamii, huelezea habari za ushujaa na mashujaa, huwasilishwa kwa kughanwa au kuimbwa pamoja na ala za muziki, hutungwa papo kwa papo yaani hautungwi kabla na kuhifadhiwa kichwani na hutawaliwa na muktadha wa utungaji na uwasilishaji kwa jamii.

Muhtasari wa Utendi

Utendi wa Rukiza (Enanga ya Rukiza) ni miongoni mwa tendi simulizi mashuhuri za  Wahaya na Wanyambo mkoani Kagera nchini Tanzania.
Utendi wa Rukiza uliimba na Yeli (manju wa tendi) aitwaye Habibu Suleiman  ambaye alizaliwa  mwaka 1929 na kufariki mwaka 1993. Utendi huu ulirekodiwa na M.M. Mulokozi mwaka 1974.

Utendi wa Rukiza ni utendi wa Kisira (Kiwasifu) unaosimulia hadithi ya maisha ya Nguli au shujaa Rukiza  kabla ya kuzaliwa hadi kifo chake matukio yanayojitokeza katika utendi huu yanapelekea kupata ruwaza ya shujaa kama ilivyoelezwa na wataalamu wa utendi na hivyo kumnasibisha Rukiza na mashujaa wa Kiutendi

Fomula zilizotumika katika  wa Utendi wa Rukiza.
Utendi wa Rukiza  huweza kuelezwa kwa fomula zifuatazo:  
Ushujaa = Ushakii + sihiri + watu
Utendi huu umefuata fomula hii kwa sababu ni miongoni mwa tendi za kiafrika ambazo nguvu za ushujaa hutegemea ushakii, sihiri na watu.
Hapa tunaona kuwa Rukiza ana nguvu zaidi za sihiri kuliko Ruhinda. Ruhinda anajaribu kumpiga Rukiza lakini anashindwa. Kushinda kwa Rukiza. hakutokani na ubora wa majeshi ya Rukiza bali kunatokana na nguvu za ziada za sihiri. Ili Kumshinda Rukiza inabidi Ruhinda naye atafute nguvu za ziada kwa waganga ambapo baadaye anafanikiwa kumshinda Rukiza kwa kugundua asili ya nguvu zake kwa kupitia kwa waganga/wabashiri.
Hivyo mapambano katika utendi huu na tendi nyingi za Kiafrika ni silaha, sihiri na watu na sihiri hushindwa kwa sihiri bora zaidi. Hapa  ina maana kuwa shujaa hufanikiwa anapokuwa na nguvu na ujasiri (ushakii), msaada wa uganga na ushirikiano na watu (Mulokozi 2002:7).

Fomula Simulizi

 Wamitila (2003:50) aneleza kuwa fomula simulizi hutumiwa kuelezea tungo ambazo hurudiwarudiwa katika usimulizi wake. Sifa hii yaweza kupatikana katika fasihi andishi na fasihi simulizi. Katika fomula simulizi mtunzi hana muda wa kupangilia yaani anatunga papo kwa papo Jadi anayotumia mtunzi imeshinikiza vipashio fulani vya lugha ambavyo mtunzi anavitumia katika utunzi wa utendi/ shairi. Kitu cha muhimu kwa mtunzi ni kuwasilisha kwa kutumia sifa za kijadi na siyo ubunifu binafsi. Hapa kinachozingatiwa ni kuimba kwa kufuata ala za muziki. Fomula simulizi ina sifa za uradidi/ urudiaji wa maneno/ sentensi, ujazaji wa nafasi wazi na uhusishi. Katika ujazaji wa nafasi mtunzi anaingiza vitu vipya na shairi linaendelea.KARATASINI Kwa kifupi ni kwamba utendi wa Rukiza umetumia  fomula simulizi kwa sababu kuna urudiaji mwingi umefanyika . Kwa mfano mishororo ifuatayo:
175: Kutokea mlimani huonekana kama madimbwi ya mvua za masika!
343 Ukiwa mlimani yaonekana kama madimbwi ya mvua za masika!.
Matumizi ya takriri katika utendi huu ni kipengele ambacho kinafanya fomula simulizi ijitokeze au itumike kwani huonyesha urudiaji wa maneno, sentensi na vifungu vingine vya maneno kwa lengo la kuimbika.

Matumizi ya Topo
Fomula simulizi katika utendi huu iliongezewa Topo ambayo ni vitushi radidi. Topo zizonazojitokeza katika utendi huu ni kama zifuatazo:
Mtoto kuongea kabla hajazaliwa, orodha ya Baganga ambao  wamekuwa wakiitwa mara nyingi, topo ya mtoto kuonyesha maajabu baada ya kuzaliwa. Vipengele hivyo huonyesha uradidi wa vitushi yaani vipengele ambavyo vimerudiwarudiwa.

Ruwaza ya shujaa
 Utendi huu wa Rukiza unaingia katika ruwaza ya shujaa kwa kuwa unamuelezea Rukiza kama  shujaa kutokana na hatua muhimu alizozipitia toka kuzaliwa hadi kifo chake.  Matukio haya ni kama yafuatayo: Kuzaliwa kwa Rukiza kimiujiza na mama yake akiwa ugenini, utoto wa Rukiza na maajabu anayoyatenda, kurejea kwa Baganga Byantanzi na vituko zaidi vya Rukiza na maajabu anayoyatenda, kurejea kwa Baganga Byantanzi na vituko zaidi  vya Rukiza njiani kustawi kwa Baganga Byantazi, ujio wa Kilokote (Kalondano) na kukaribishwa kwake katika ukoo wa Baganda, usaliti wa Kilokote, pambano la kwanza kati ya Ruhinda na Rukiza na kushindwa kwa jeshi la Ruhinda. Juhudi za Ruhinda ya kutafuta ushindi kwa njia ya sihiri kuolewa kwa binti Rukiza na Ruhinda, kufichuliwa kwa siri ya uwezo wa Rukiza na binti yake kutokana na athari ya sihiri. Pambano la pili kati ya Ruhinda na Rukiza kifo cha Rukiza na mwishoni ni kifo cha Ruhinda kwa mkono wa mkewe   aliyelipiza kisasi.

Fani na maudhui katika Utendi wa Rukiza
Fani
Hiki ni kipengele muhimu sana katika kuchambua kazi yoyote ya fasihi. Katika fani tutaangalia vipengele vifuatavyo.
i) Mtindo, (ii) Lugha (iii) Wahusika  (iv) mandhari

 

 Mizani
Kwa kiasi kikubwa utendi huu hauna mizani ndefu lakini kuna baadhi ya mistari michache imejitokeza kuliko mingine amabayo ina mizani ndefu. Kwa kutumia muundo wa mizani ndefu kuliko mizani ya kawaida,  kumeleta mchomozo katika utendi huu. Pia mtunzi alikuwa na nia ya kusisitiza jambo fulani kwani mishororo iliyoelezwa hapa chini:
92: Jamani mtoto gani huzungumza akiwa tumboni mwa mama yake!
111: Nikaona dume huyo anaanguka mweleka karibu na muoto
115: Waliporudi walikuta kimekwisha mchinja dume kwa vidole vyake.
254: Kikajibu, Nimetokea katika nchi ya Wasiovaa na   Wasiojifunika
343: Ukiwa mlimani yanaonekana kama madimbwi ya ya mvua za masika!

Mtindo
Katika mtindo wa utendi huu kuna matumizi ya majigambo, sitiari, usambamba, takriri, tashbiha na matumizi ya chuku.

Majigambo
Katika utendi huu mtunzi ametumia mtindo wa majigambo katika usimulizi wake kwa mfano katika mishoro 23-36 akasema “Nilizaliwa ndimi Rukiza. Hapa Rukiza anaanza masimulizi kwa kujigamba kama yeye ni shina la mgomba lililooza. Hapa inamanisha mfumo anaouwakilisha umeoza lakini hataanguka peke yake utamwangusha na yule atakayeuchokoza. Pia anajigamba kwamba yeye ndiye Rukiza mkombozi wa kaya ya Baganga ambaye ndiye msingi na mleta ngoma na asali.


Matumizi ya Sitiari
Sitiari hutumika kufananisha vitu viwili kwa kutumia neno “ni”. Katika utendi huu mtunzi amaetumia sitiari pana. Kwa mfano katika mishororo ifuatayo kuna matumizi ya sitiari
Mshororo wa 34-37 pale Rukiza anapojifananisha na shina la mgomba kwa kusema
            “Mimi shina la mgomba nilioza zamani
            Nilikataa kuanguka bila kutikiswa atakayenitikisa nitaanguka naye”
            Pia katika mishororo ifuatayo kuna matumizi ya sitiari
89:       Wakasema, “Huyu si mtoto, labda ni kioja, ni ndumba
504:     Hawa ni njiwa tu, nitawatumia
Katika sitiari hiyo ya shina la mgomba, Rukiza anaonyesha jinsi anavyojiamini na  nguvu alizonazo. Yeye hapa anatabiri kifo chake kwani alijua siku moja atakufa na yule ambaye atamuua na yeye atakufa naye.

Matumizi ya Tashbiha

Hii ni tamathali ya semi ambayo vitu viwili hulinganishwa kwa kutumia neno “kama”. Katika mshororo wa 186 hapa mtunzi alitaka kulinganisha uwezo wa pande mbili Kwa mfano,
186: Wanaume kadhaa kama ninyi hapa tulikuwepo
Tashbiha nyingine ni kama zifuatazo:
200: Sitopata tena uzao kama huu
203: Ana roho kama jiwe
347: Anasema yeye ni mfalme kama wewe.

Usambamba
Hii huonyesha mfanano wa mistari miwili, mitatu na kuendelea. Mf katika mishoro ifuatayo
608:Eeee eeee ai maskini
609:Eeeee ai maskini

Matumizi ya chuku
Katika utendi wa Rukiza kuna matumizi ya chuku yaani maneno yenye kutia chumvi. Kwa  mfano katika mishororo ya 172-179 tunaona kuna matumizi ya chuku. Kwa mfano:
Badanga wakapona ufukara
Wakanywa maziwa yakawashinda
Mengine wakayamwaga katika ishazi kutokea mlimani huonekana kama madimbwi ya mvua za masika!
Tukaona samli ngumu
Nyumbani mwa Rukiza ikichezewa na watoto
Nikaona samli laini inakandikwa kwenye viambaza
Bagnga wote wakatonoka

Katika hali ya kawaida haya hayawezi kutokea kwa hiyo hapa kuna ukuzaji/kutia chumvi. Hapa mtunz alikuwa anataka kukusisitiza jambo fulani kwamba mambo yaliyokuwa yakitendeka hayakuwa ya kawaida.

Takriri
Kurudiarudia kwa maneno  kunaonyesha msisitizo wa jambo fulani yaani mtunzi anataka ujumbe fulani uifikie jamii. Kwa mfano
95:       Wakajaribu vyembe vya mlanzi vikateleza
96:       Wakajaribu kisu cha kunyolea hakikufaa
460:     Ewe Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza, mtoto wa mama
600:     Nyingine ipo kwenye mgomba wa ntundu
601:     Nyingine ipo kwenye muoto wa mtoto

Udokezi
Udokezi hutegemea muktadha katika utendi wa Rukiza mtunzi ametumia udokezi akiamini kuwa hadhira inaelewa kile anachokisema kwa kudokeza kwa mfano katika mshororo wa 441. “Vipi cheupe –cha-wamala hii ina maana kuwa ng’ombe wake ni mweupe. Hapa anadokeza kitu kingine na inawakilisha kisakale. Kwa hiyo wenye utamaduni wa Kihaya wataelewa kinachozungumzwa.

Lugha
Lugha katika utendi wa Rukiza imeonekana kueleweka zaidi kwa wazee kuliko vijana/watoto. Sababu kubwa zaidi ni mtindo wake unaotumia mbinu mbalimbali za lugha hususani tamathali za semi kama  sitiari, jazanda, takriri, ishara na udokezi katika kuwasilisha ujumbe  wake. Mwimbaji  wa utendi huu amechukulia kuwa hadhira yake inafahamu vyema matukio yanayozungumziwa.

Lugha ya Kifalme
Kuna maneno yanayotamkwa kabla ya kutaja jina la mfalme. Kwa mfano mishororo ya (329-
329: Kikasalimia, Na uishi na kudumu milele ee Mfalme!
335: Ewe mtukufu mimi nilifika kwa Rukiza
330: Kikasujudia miguuni kwa mfalme
376: Mfalme akajibu, Kitwana hufa hutokufa
378: Kwa kudhubutu kubomoa uzio wa mfalme kama huu
379: Maana ni muhali kwa uzio wa Mfalme kuvunjwa na mtwana

Kwa hiyo lugha ya kifalme imetumika kuonesha namna utawala wa kijadi ulivyokuwa na nguvu na pia ilitumika kuwagawa watu katika matabaka kutegemea namna walivyo thaminiwa katika jamii.

Lugha ya ufugaji/ng’ombe
Sajili ya ufugaji ina maneno na misemo mingi inayohusu ng’ombe mfano mzuri ni  majina au maneno yanayowatambulisha  ng’ombe kwa mujibu wa rangi na sifa zao nyinginezo zinazoonekana. Kwa mfano kisa/rusa ng’ombe mwenye rangi ya maziwa au krimu. Siina – ng’ombe mwenye rangi ya kahawia nyeusi kitale – ng’ombe mweupe kabisa, Gaaju – ng’ombe mwenye rangi ya kahawia nyepesi, Bihogo – ng’ombe mwenye rangi ya kahawia nyeusi, Nkungu- ng’ombe asiye an pembe

435:     Milia wa ikondo – ng’ome mwenye pembe kubwa na ndefu zilizoelekea mbele

Lugha ya kijadi
Matumizi ya maneno ya kijadi (uchanganyaji misimbo maneno ya kiswahili na Kihaya)
Katika utendi huu kuna maneno ya kijadi ambayo ni vigumu kuyafasiri katika lugha ya kiswahili. Mfano muhoro – panga la kijadi
419:  kilele          - kibuyu cha kunywea pombe chenye shingo ndefu ambacho hutumiwa na wanaume hasa wanaoheshimika.
660:  Nchweke:  Pepo au mashetani yanayompata mtu aliye karibu sana na yule aliyefariki .
87: na 89 Ekikumila:   Kisifa cha mapepo/ jini au mazingaombwe
587:  Kilela -      Kitovu cha mtoto mchanga
600: Ntundu       Aina ya mgomba, ndizi zake hutumika kutengenezea pombe
16-17  Eshwiga -         Mboga ya majani ambayo huliwa na pia hutumika kama dawa (mnavu)
111:   Ekome/komi -   Moto unaokokwa mbele ya nyumba wakati wa usiku na kuzungukwa na wanaume wakati wanaongea. Mara nyingi hukokwa wakati wa msiba (matanga) au wafugaji wanapotumia kuulia wadudu.
126:  Ekigabilo:  Mti mkubwa wa baraka, ambapo watu hufanya matambiko ili kukamilisha mambo yao.
16-17 Omugobe:  Majani ya kunde, omushonge: nyumba ya jadi ya wanyambo
         Eshwiga – mboga ya majani ambayo huliwa na pia hutumika kama dawa (mnavu)
11:   Obuganga: Nchi ya Baganga
Obukhankabana:  Visumba vya ndizi
Ekyanzi – Gudulia la mti la kukamulia maziwa
Engozi – mbeleko ya ngozi
Eiyembe – kioja pembe ya uchawi au mazingaombwe yenye vituko
251:  Mkago:  ndugu wa kuchanjiana damu (kushela mkundi)

Yapo maneno mengi sana ya kijadi ambayo yametumika katika utendi huu. Hivyo huu ni uchanganyaji misimbo wa lugha ya Kiswahili na Kihaya ambapo baadhi ya  maneno yanapaswa yatafsiriwe ili kuufanya utendi huu ueleweke zaidi. Mhariri amefanya hivyo mwisho wa utendi huu.
Lugha ya Uganga
Lugha hii ya uganga imetumika pale Ruhinda alipoita wabashiri ili wamfanyie dawa binti wa Rukiza na familia yake mfano katika mishoro ifuatayo, lugha ya uganga imetumika mfano katika mshoro wa 537-589.

537: Wakapiga ramli, utumbo wa kuku ukawa mweusi
538: Wakapiga ramli bila mafanikio
581:  Tumetakasa Ndumba  -Ahamari
582: Kaya yote ya Rukiza ihamishwe
583: Tumetakasa Ndumba Paramizi
584: Kaya yote ya Rukiza iparamiwe!
586: Mpe mwali ndumba hizi
587: Azitundike kwenye nguzo tatu za kilele
588: Akikuuliza unamzindika kitu gani
589: Mjibu kuwa umemzindika dhidi ya mapepo ya mizimu ya kwao
Lugha hii inaonesha matumizi ya maneno ya uganga yanayohusiana na sihiri.
            Vilevile lugha ya dini imetumika kwa kiasi kidogo, kwa  mfano katika mishororo ya 563 na 569; Akajibu “Mungu anipishe mbali” Hapa inaonesha imani ya kidini ya mwali huyo.  (binti Rukiza). Kwa ujumla lugha iliyotumika katika utendi huu ni ya kawaida japokuwa kuna mchanganyiko wa maneno  ya Kihaya lakini inaeleweka.
                                                                                                                                        
Wahusika
Rukiza              
Ni mhusika mkuu katika utendi huu na ndiye amebeba jina la utendi. Alizaliwa ili kuwaokoa Baganga baada ya kupata njaa kali huko Uganda na kulazimika kuhamia Karagwe kutafuta malisho na makazi yao. Rukiza maana yake ni mkombozi na kweli amewakomboa Bananga japo alizaliwa kimaajabu sana. Alikuwa na nguvu za ajabu zilizotokana na sihiri, kiasi kwamba alivyokuwa akichomwa mkuki hafi na badala yake anaua watu wengi sana alipopigana na Ruhinda.  Binti yake aliolewa na Ruhinda na baadaye alikuwa chanzo cha kifo cha baba yake. Kuzaliwa kwake kulionekana kioja kwa watu wote.  Hii ni kutokana na matendo aliyokuwa akiyafanya akiwa tumboni na mara baada ya kuzaliwa.

Vilevile Rukiza anaamini sana imani ya jadi hasa kufanya matambiko na mambo  mengine ya mila na desturi. Aliweza kufanya mambo ya ajabu ambayo waheshimiwa wengine na wafalme walikuwa hawayafanyi kwa mfano kuishi na Kilokote (Kalondano) ambaye alikuwa ni mtwana.  Hata hivyo kilokote ndiye aliyekuwa chanzo cha mapigano kati ya Rukiza na Ruhinda na hatimaye wote wakafa. Hii ilitokana na maneno aliyoyasema Rukiza mwenyewe kuwa atakayemtikisa ataanguka naye. Hata hivyo Rukiza anaonekana ni tu mwenye busara kwani alipanga kwenda kwa mfalme Ruhinda kuuliza juu ya maneno ya uchonganishi aliyoletewa na Kilokote. Kabla hajafanya hivyo alivyokusudia ndipo usiku huo huo akavamiwa na Ruhinda na vita ikaanza.

Ruhinda
Alikuwa mfalme wa Karagwe ambaye aliwapokea Baganga walipohamia kutoka Uganda wakitafuta makazi na malisho ya ng’ombe. Mwanzo alikuwa mtu wa karibu sana na Rukiza na walikuwa wakishirikishana mambo mbalimbali kama marafiki ila anakosa busara anapoletewa maneno ya uchochezi na Kilokote. Alipaswa kumwuliza Rukiza juu ya yote aliyoambiwa na Kilokote, badala yake anaenda kuvamia kwa Rukiza kwa mapigano na anapigwa vibaya sana na Rukiza na watu wake aliambatana nao wengi walikuwa mfano katika mishororo (451-427). 
Alimwoa binti Rukiza kama mbinu ya kujua asili ya nguvu za Rukiza baada ya kuambiwa na wabashiri wake (wafumu). Baada ya kumwoa binti Rukiza aliendelea  kuwatumia hadi wakafanikiwa kumfanya huyo binti Rukiza aseme asili ya nguvu za baba yake na ndipo alipopigwa na Ruhinda  na jeshi lake na kumuua. Hapo walichukua ng’ombe wote wa Rukiza na kuja nao. Binti yake naye akamchoma kisu Rihinda naye akafa kwa kujikata shingo. Mfano katika mishororo (630-683).

Kilokote
Ni mtwana ambaye aliishi kwa Rukiza baada ya kuokotwa njiani akiwa uchi. Alipokutwa njiani Rukiza  alitaka kumwua ila Baganga wakakataa na ndipo Rukiza akaamua kumchukua akakaa naye. Kilokote alipendeza na kunawiri nyumbani kwa Rukiza.
-          Alikuwa chanzo cha mapigano kati ya Rukiza na Ruhinda kwani ndiye aliyewachonganisha hadi mapigano yakaanzishwa na Ruhinda.
-          Alivunja mihoro na kilele alipotumwa kwa Ruhinda na Rukiza ili visionekane kule kwa Rukiza. Akiwa anaingia kwa Ruhinda alipitia Buyondo na Wayondo wakataka kumuua, akajitetea na ndipo alifika kwa mfalme Ruhinda na kuongea uongo ambao ulileta mgogoro. Mfano katika mishororo (395-419).
Baada ya kutaja mali zake zote alizodai zimeharibia huko kwa mfalme Ruhinda, Rukiza alimpa nyingine naye Kilokote akaingia ndani akalala baada ya kula na usiku ule vita ikaanza.

Binti Rukiza
Aliolewa na Ruhinda baada ya Ruhinda kutumia nguvu za sihiri kwa kuwatumia watabiri ambao walitumia dawa zilizomfanya Rukiza kukubali bintie kuolewa na Ruhinda.
Hata hivyo sihiri hizo zilitumika pia kumfanya Binti Rukiza atoe siri ya nguvu za baba yake.
Baada ya baba yake kuuawa, analipiza kisasi kwa kumchoma kisu Ruhinda naye kujikata shingo na ndipo usemi wa baba yake wa atakayenitikisa nitaanguka naye ulipotimia mshororo wa 36).
Wahusika wengine wametajwa na mtambaji katika kukamilisha utendi huu. Wahusika hawa ni kama Kachenkela ambaye ni mama yake Rukiza. Wayondo ambao ni wapishi wa mfalme Ruhinda, majeshi ya Ruhinda watoto wengine wa Rukiza na mke wa Rukiza (Luhunge binti Nshaiga).

Mandhari
Mandhari ya utendi huu ni katika jamii za Wahaya na Wanyambo katika mkoa wa Kagera nchini Tanzania. Matukio yaliyomo katika Utendi wa Rukiza yalitokea katika ufalme wa Karagwe jamii ya Baganga ambayo imehamia Karagwe kutoka Kaskazini ya Uganda na magharibi ya Rwanda. Jamii hii ni ya wafugaji ambao walizunguka kutafuta malisho ya mifugo yao mpaka wakafika kaskazini Magharibi mwa Karagwe na kujenga makazi yao katika eneo la Byantanzi.

Maudhui ya Utendi Wa Rukiza
Utendi wa Rukiza unaakisi mgogoro wa kihistoria kati ya mifumo miwili yaani mfumo wa kijadi na mfumo wa kifalme. Amali za mfumo wa kijadi ni umoja na ushirikiano wa watu wa damu moja, matambiko ya pamoja, umiliki wa mali kwa pamoja hususani mifugo na ardhi, uamuzi wa pamoja wa masuala muhimu ya kiukoo na wajibu wa kulindana na kutunziana siri za ukoo.
Katika kuangalia maudhui ya utendi huu tutajikita katika vipengele vya motifu, dhamira  na migogoro.

Motifu
Motifu ya mtoto wa ajabu.
Kuna Motifu ya mtoto wa ajabu ambaye ni Rukiza. Amezaliwa katika mazingira ya ajabu. Alikuwa anaongea akiwa tumboni mwa mama yake amemlazimisha mama yake amtayarishie vitu fulani kabla hajazaliwa na anamlazimisha mama yake amzae. Hii inajidhihirisha katika mishororo (20-22, 40-45 70-71). Karibu nitazaliwa, ndimi Rukiza,      Jina langu niite Rukiza

Motifu ya mtoto wa ajabu inaelezewa pia katika mishororo  ya (70-139). Kwa kuangalia mishororo hiyo hapo juu tunaona kuwa Rukiza ni mtoto wa ajabu, kwa sababu ana matendo ya ajabu ambayo hayatarajiwi kufanywa na mtoto wa umri wake. Hii imepelekea jamii yake ya Baganga kusema:
87:       Wakasema, Huyu si mtoto, tumeona kioja!”
            Hii ni kutokana na matendo aliyoyafanya ambayo si kawaida.

Motifu ya Safari
Hii inajidhirisha katika utendi huu, kwa safari ya Baganga walipokuwa wakitoka Kaskazini mwa Uganda kuja Karagwe kwa ajili ya kutafuta malisho ya ng’ombe wao. Inaelezwa kuwa Baganga walivuka mto kuja Kaskazini mwa Karagwe.

Motifu hii ya safari inapelekea kuwa na motifu ya msako ambapo jamii ya Baganda inasafiri ikisaka malisho ya ng’ombe wao na makazi yao kwa sababu kule walikotoka kulikuwa na njaa na ukame. Hii inajidhihirisha katika mishororo ya (136-162).
136; Akasema ,Nibebeni turudi kwetu
137: Baganga wakambeba mtoto
138: Siku hiyo Baganga wakambeba mtoto
139: Tukakongozana nyianyianyia!
141: Tukafika kwenye ziwa la chumvi
161: Nikaona wamemvusha Rukiza
162: Akaja kwao Byantazi
Katika safari yao ya kusaka malisho na makazi bora, tunaona kuwa walifanikiwa kufika Byantazi ambapo walipata neema kama inavyodhihirisha katika mishororo ya (170-174).
170: Wakatamalaki na kumjenge kitala
171: Ukawa ufalme kama falme nyingine
173: Baganga wakapona ufukara
173: Wakanywa maziwa yakawashinda
174;Mengine wakayamwaga katika ishazi

Dhamira
Dhamira kuu katika utendi wa Rukiza ni mgogoro uliosababishwa na ujenzi wa himaya mpya  ambayo imeleta mgogoro wa kihistoria na wa kitabaka kati ya mifumo miwili yaani, mfumo wa kijadi / kiukoo  na mfumo mpya wa kifalme wa dola inayoinuka. Mgogoro huo ni wa kimfumo aamabapo kuna mapambano ya kiukoo inayowakilishwa na Ruhinda na ule wa kifalme unaowakilishwa na Rukiza.

 Dhamira nyingine ndogondogo   zilizojitokeza  ni kama zifuatazo:
Usaliti: Hii inajitokeza pale ambapo binti Rukiza alivyomsaliti baba yake kwa kutoa siri kuhusu nguvu zinazomlinda baba yake. Siri hiyo anapewa mfalme Ruhinda ambaye anapanga njama za kumwua Rukiza. Uvujaji wa siri hiyo unasababisha kuuawa kwa Rukiza. Hii imeonekana katika mishororo (598-629).

Usaliti mwingine unajitokeza pale ambapo Kilokote anapomsaliti mfalme Rukiza wakati alipotumwa kupeleka salamu kwa Ruhinda alimtaka ashiriki katika ufunguzi wa nyumba Byantanzi hapa anatoa maelezo ambayo hajatumwa. Hii imeonekana katika mishororo ya (335-349).
335:Ewe mtukufu, mimi nilifika kwa Rukiza
336: Nikiwa na ng”ombe wangu magana sitini
337: Akaninyang”anya na kuwachukuwa
338: Ameleta halaiki ya watoto wa kwao
339: Na kuwajaza katika uwanda mzima
345: Nyumbani kwa rukiza inachezewa na watoto
346: N samli laini inakandikwa viambazani
347: Anasema yeye ni mfalme kama wewe
348:Hakutaaadhimishi bali anakuamkua
349: Hata kigoda anakalia cha mapembe

Sihiri
Katika utendi wa Rukiza suala la sihiri limeonyeshwa kwa kiasi kikubwa kwani kuna matumizi ya uganga katika kuwezesha mambo fulani kufanyika. Hii inajidhihirisha  pale ambapo Ruhinda alitaka kujua asili ya nguvu za Rukiza na Rukiza alipokataa binti yake kuolewa na Ruhinda. Wakaona kwamba njia pekee  ya kufanya hilo lifanikwie ni kumwita mbashiri. Huu inajidhihirisha katika mishororo ya (533-595).
533:  Ruhina akasema, ‘Niiteni mbashiri wangu”
535:  Mfumu huyo alikuwa akiishi Byantazi
            536: Wakakamata kuku Mchakuraju-Mkeshaji
537: Wakapiga ramli, utumbo wa kuku ukawa mweusi
538: Wakapiga ramli bila mafanikio
581:  Tumetakasa Ndumba  -Ahamari
582: Kaya yote ya Rukiza ihamishwe
583: Tumetakasa Ndumba Paramizi
584: Kaya yote ya Rukiza iparamiwe!
586: Mpe mwali ndumba hizi
587: Azitundike kwenye nguzo tatu za kilele
588: Akikuuliza unamzindika kitu gani
589: Mjibu kuwa umemzindika dhidi ya mapepo ya mizimu ya kwao
           
Sihiri au suala la uganga linatokana na imani kwamba ili kufanikisha jambo fulani ni lazima  utumie sihiri. Katika utendi huu, ukiwa mmojawao wa tendi za Kiafrika, mashujaa wengi husaidiwa na nguvu za sihiri pamoja na miungu yao. Mfalme Ruhinda alifanikiwa kumshinda Rukiza kwa sababu ya kutumia sihiri ambayo ilifanya binti kutoa siri za nyumbani kwao hasa siri ya nguvu za baba yake.

Dhamira ya kulipiza kisasi
Kulipiza kisasi kilitokea kati ya mfalme Ruhinda na Rukiza ambao walikuwa katika mgogoro mkali uliosababishwa na Kilokote ambaye alitoa taarifa  za ugombanishi aliporudi kutoka ikulu ya Ruhinda. Aliporudi kutoka Ikulu Rukiza akamuuliza mfano katika mishororo ya (405-418)
Rukiza alikasirishwa na maelezo yaliyotolewa na Kilokote akapanga kwenda Ikulu kumuona Ruhinda. Hii inaonyeshwa katika mishororo ya 427-429

Katika utendi huu ulipizaji wa kisasi unajitokeza pale ambao mshikamano wa kiukoo unadai ulipizaji kisasi iwapo mwana koo mmojawapo anadhulumiwa au kuawa. Kanuni inayotawala katika utendi huu ni jicho kwa jicho. Hii inaidhihirisha pale mfalme Rukiza  anapouawa inabidi binti yake alipize kisasi kwa kumuua Ruhinda. Hii inajidhihirisha katika mishororo ya 679-683

Dhamira ya uzazi
Hii imejitokeza kwenye mshororo wa 181-184 na 200-205 katika mishororo hii suala la uzazi inaonyeshwa pale Rukiza amekua akaoa na kuwa na familia, vile vile katika mshororo wa 200-205 baada ya Rukiza kupata watoto. Hapa inaonesha jinsi uzazi ulivyo muhimu.

Dhamira ya utabaka unyanyasaji na dharau
Utabaka umeonyeshwa kwa kiasi kikubwa katika utendi huu. Kwani jamii hii ya Baganga imegawanyika katika matabaka mawili tabaka la kifalme na tabaka la watwana ambalo ni la watu wa chini.
Mfumo wa kiukoo wa Rukizia ni wa kitabaka Rukiza anatamba kuwa haitwi “Rukiza” bali huuitwa Mwinyi na kwamba yuko radhi kufa kuliko kula takataka. Hii inajidhihirisha katika mishororo ya (462-463).
462: Ni nani wewe uniitaye “Rukiza ?”
463: Hujui kuwa mimi huitwa “Mwinyi”

Kwa kuwa Rukiza alikuwa mfalme yaani mtu wa tabaka la juu hakuweza kuchanganyika na watwana. Inafikia wakati chakula wanachokula watu wa tabaka la chini. Kwa mfano katika mishororo ya (16-18). Heri nijiue kuliko kula haramu. Kula mboga za majani ya kunde na shiviga kula takataka zisanywazo na wajakazi.

Lakini utabaka wa jamii hii haujakoma, bado unawezekana kwa mtwana kugeuzwa mwana-ukoo kama inavyotokea kwa Kilokote ambaye ni mtwana. Kilokote ananusurika kufa kwa sababu ya utwana wake, kwani watwana walikuwa wakitolewa kafara katika jamii ile. Hali hii ya utabaka kwa kulitenga tabaka la chini inajidhihirisha kwa maneno ya mwimbaji Habibu Selemani  ambaye kila wakati anatahadharisha hadhira yake ijihadhari na watwana. Hali hii inaonyesha jinsi utabaka ulivyokuwa wa hali ya juu. Hii  inajidhihirisha katika mishoro (303-308).
Lakini ogopeni mtwana!
Mzee Yoweli, muogope mtwana!
Kweli ogopeni kitwana kama mimi hapa!
Ha! Ha! Ha! Ha!
Yarabi maskini!
Lakini ogopeni kitwana!

Kutokana na utabaka huo watwana ambao ni wa tabaka la chini  walifikia hata kuawa kwa mfano mishororo 166-169.
Nipo alaipokutana na mtwana.
Akavuta upinde asubuhi na kumwua kwa mshale.
Watu wakauliza, “Rukiza, mbona umemwua mtwana?”
Akajibu,” Hiyo ni sadaka ya kaya yetu.

Pia katika mishororo (206-209) inaelezea jinsi watwana wanavyoendelea kunyanyaswa na kuonewa na kudharauliwa.
Tukakuta kitwana kimoja kimeanguka kichalichali
Kimejifunika uchi wake kwa vidole
“Hebu mwueni mtwana huyo!”
Toka, Rukiza atakuua!”

Mtwana huyu aliponea chupuchupu baada ya kusema kuwa ana uhusiano na Rukiza.  Hii inaonyeshwa katika mishororo (211-215) mbona mimi ni mchale wa Rukiza.
Pia utabaka unyanyasaji na dharau haviishii tu kwa watwana, inaendelea hata kwa kabila ya Wanyambo. Kwa mfano katika mishoro ya (141-158) tunaona kwamba watu hawa wananyanyaswa  na kudharauliwa. Hii inajidhihirisha kwa kuangalia matumizi ya “ki na vi”ambayo yanaonyesha kudhalilisha mtu au kumdharau mtu. Kwa mfano:
Tukafika kwenye ziwa la chumvi
Tukakuta vinyambo
Vimekaa vinachunga mwaro
“Vinyambo nipisheni niende zangu!”
Vinyambo vikakataa, “oya”
Enyi vinyambo, “Tokeni nipite!”

Hapa inaonyesha utabaka na dharau kwa tabaka la chini hasa watwana na Wanyambo. Dharau na utabaka huo unajidhihirisha kwa matumizi ya kiambishi  -ki ambacho ni cha awali cha nafsi kinachoonyesha umoja. Dhana kubwa inayopatika hapa ni udogoshaji yaani kitu kinashushwa hadhi.

Dhamira ya Mila na desturi
Katika utendi huu kuna baadhi ya mila na desturi ambazo zimeonyeshwa. Kwa mfano matambiko, hii inajidhihirisha katika mishororo ay 211-214. Hapa inaonesha mila ya kuchanjiana ili kujenga undugu mbona mimi ni mchale wa Rukiza huyo Rukiza mnayemzungumzia tujidumiliza tulichangiana kule Byantanzi tulipokuwa wadogo tukichunga na ndama wa kijivu.
Mbona mimi ni mchale wa Rukiza?
Huyo rukiza mnayemzungumzia tumedumiliza
Tulichanjiana kule Byantanzi
Tulipokuwa wadogo tukichunga ndama wa kijivu
Pia katika mila na desturi ilikuwa ni mwiko kutoa siri za familia kwani waliamini kuwa inaweza kusababisha matatizo kwenye familia.
 Kwa mfano tunaona pale Binti Rukiza alivyotoa siri ya nguvu za baba yake kwa Ruhinda tunaona kuwa ilisababisha kifo. Pia tunaona ilikuwa mila na desturi kuheshimu nyumba ya mfalme hasa jikoni kwa mfalme. Ilikuwa ni mwiko kwa mtu kwenda au kupitia Buyondo yaani jikoni kwa mfalme.

Migogoro
Mgogoro mkubwa katika utendi wa Rukiza ule kati ya Rukiza na mfalme Ruhinda, ambao umesababishwa na migongano ya mifumo ya kijamii unaowakilishwa na Rukiza na ule unaowakilishwa na Ruhinda. Mgogoro huu unapelea kutokea kwa vita baina yao baada ya kuchonganishwa na kitwana (Kilokote) ambaye alitumwa na Rukiza kupeleka salamu kwa Mfalme Ruhinda naye akabadili maneno  kwa kuongea uongo, mfano katika mshororo wa 144-158.

Mgogoro mwingine ni kati ya binti Rukiza na mfalme Ruhinda. Baada ya Rukiza kuuawa na mfalme Ruhinda bintiye Rukiza ambaye ndiye aliyesababisha kifo cha baba yake baada ya kutoa siri  tunaona Binti Rukiza anachukua kisu na kumuua mfalme Ruhinda  rejea katika mishoro ya (645-685).
Vilevile katika utendi huu kuna migogoro mwingine midogo midogo kwa mfano mgogoro kati ya Rukiza na Vinyambo, mishororo ya (144-158) pale Vinyambuo walipofushwa macho baada ya kumzuia Rukiza kuvuka ziwa Chumvi alipokua akielekea Byantanzi.
Pia kuna mgogoro kati ya Kitwana (Kilokote) na mfalme Ruhinda, baada ya Kilokote aliyekuwa mtwana wa Rukiza  kutumwa kwa mfalme Ruhinda naye badala ya kupita katika lango kuu akatoboa ua na kuingia ndani ya miliki ya mfalme na kusababisha mfalme Ruhinda kuchukia mfano mishororo ya (369-379).
Mgogoro mwingine uliojitokeza ni kati ya Rukiza na Kitwana Kilokote ambapo Kilokote alipiga kelele na kuwatisha watoto wa Rukiza ambapo walitetemeka kwa hofu na kuutisha baba yao mfano katika mishororo ya (206-239).
Kwa hiyo migogoro iliyoibuliwa katika utendi huu ni kwa lengo la kuonesha utabaka uliokuwemo katika jamii pamoja na ushujaa ulivyojidhihirisha kulingana  na nguvu za sihiri zilizoambatana na  maajabu mengi.

Uhusiano wa utendi wa Nyakiruukibi na tendi nyinginezo
Mfalme Edipode/FUMO LIONGO(ulijali)RUKIZA(DUMILIZA)
Hii inahusiana na utendi wa Nyakiirukibi katika suala la mtoto wa balaa(nuksi)Edipode mwenyewe alitabiliwa na baba yake kwamba atakuwa mtoto wa nuksi na ndio maana akaenda kutupwa
Kwa ufupi tunaweza kusema kuwa utendi wa Rukiza una uhusiano mkubwa na tendi nyingine za Afrika kwani inafuata ruwaza au sifa za tendi za Kiafrika ambazo ni ruwaza ya shujaa ambaye anatoka katika tabaka la juu, mwenye ujasiri nguvu za sihiri urijali na anayeungwa mkono na watu. Tendi hizo nyingine za kiafrika ni kama vile Silamaka, Mwindo, Lianja na Sundiata.  Mfanano huu pia unajidhihirisha katika maudhui kwani tendi nyingi za Kiafrika zinazungumzia masuala ya migogoro, usaliti, mila na desturi za Kiafrika na dhamira nyinginezo.
Uhusiano huu pia unapelekea tendi nyingi za Kiafrika kufuata fomula au ruwaza ya USHUJAA = Ushakii + Sihiri + watu.

Utendi wa Silamaka

Ukiangalia utendi wa Silamaka, ni utendi unaoelezea mapambano makali kati ya Silamaka na Maadui zake yaani Wasegou. Alikuwa mtoto a mfalme wa Fula na alisaidiana na mtumishi wake Pullori ambao walikuwa pamoja. Hatimaye Silamalamaka anauawa na albino kama ilivyotabiriwa.

Utendi wa Sundiata

Katika utendi wa Sundiata, Sundiata alizaliwa kiwete na mwenye matatizo mengi na alikuwa hana nguvu.  Baadaye alikuja kupata nguvu akawa askari mashuhuri aliyeongoza mapambano  ya kijeshi na akashinda.  Alipambana na mtu aliyeitwa Sujmunguru ambaye anatafuta siri ya kumuua Sundiata anashindwa kuipata sihiri inafanya kazi kuba sana katika utendi wa Sundiata. Tunaona baadaye Sundiata anashindwa na Sumanguru baada ya siri ya nguvu zake kujulikana.

Utendi wa MwindoKARATASI/
Katika utendi huu kunakuwa na mapambano kati ya mtoto na baba yake, Mwindo (Kabutwakunda) ambaye ni mtoto wa ajabu aliyetembea baada ya kuzaliwa ambaye anaongea akiwa bado tumboni mwa mama yake na anatembea mara tu alipozaliwa. . Utendi huu wa Mwindo unahusu motifu ya mtoto wa ajabu. Huu unahusiana kwa kiasi kikuba na Utendi wa Rukiza   kwa sababu zote zinaelezea motifu ya mtoto wa ajabu.

Utendi wa Lianja
Lianja ni utendi wa  Kongo ambao unahusu kabila la Wamongo.  Lianja anashirikiana na dada yake kuongoza Wamongo.Lianja amezaliwa katika mazingira ya ajabu yeye anatumia viumbe mbalimbali katika kupambana.
Baada ya kuangalia baadhi tendi za Kiafrika, ni dhahiri kwamba tendi hizo zina husiana kwa kiasi kikubwa sana kwani zinafuata ruwaza ya ushujaa ambayo ni ushujaa ushakii + sihiri + watu. Ila kwa kiasi kikubwa sana Utendi wa Rukiza unafanana na utendi wa Mwindo.

Hitimisho                                                                                                                       
Kwa kuhitimisha tunaweza kusema kuwa utendi huu ni wa kijadi ambao unazungumzia kwa kina tawala za kijadi za Wahaya huko Kagera  hasa wilaya ya Karagwe. Ujadi huo unaendana na ufungaji pamoja sihiri zinazowawezesha wafalme kufanikisha mambo yanayoyapangwa ili kuweza kupata ushujaa. Kwa vile utendi huu unahusu jamii ya Wahaya ndio maana kuna maneno ya kijadi ya Kihaya ambayo  yametafsiriwa ili kurahisisha uelewaji kwa wasomaji.

Kimsingi, utendi huu unahusu itikadi ya kitabaka ya kijadi ya jamii zinazohusika, ontolojia ya jamii hizo kuhusu maisha na mipaka ya uwezo wa mwanadamu, na mtazamo wa jumla wa jamii hizo kuhusu udugu na ushujaa. Pia unaakisi mgongano wa kihistoria uliokuwapo kati ya mifumo ya kijamii na kati ya matabaka yanayoiwakilisha. Utendi huu unaeleza kuwa, kwa mtazamo wa kijadi kuhusu ushindi wa jambo lolote unategemea nguvu za sihiri. Hata hivyo nguvu za sihiri zinazidiana ndio maana Ruhinda kwa kutumia wafumu (waganga) aliweza kumwua Rukiza kwa vile alitegemea nguvu za mazindiko yake aliyokuwa ameyaweka katika sehemu tofauti tofauti katika mazingira yake yaliyoishi. Mwishoni tunaweza kusema kuwa mtu wa karibu ndani ya familia anaweza akakutenda jambo baya sana kwa kutoa siri na kukusaliti kama ilivyo kwenye utendi huu. Kwa hiyo utendi huu
unafundisha kwamba siyo vizuri kutoa siri za familia kwani inaweza kuleta madhara.

                                                            MAREJEO


Finnegan, R. (1970) Oral Literature in Africa. Clarendo Press, Oxford

Mulokozi, M.M (1996) Fasihi ya Kiswahili :Chuo Kikuu Huria cha Tanzania

Wamitila K.W (2003)  Kamusi ya Fasihi Istilahi na Nadharia : Focus Publication Ltd


Mulokozi, M.M (2010) Utendi wa Rukiza :Tendi Simulizi na Andishi za Kswahili

No comments:

Post a Comment

syliverymanyama@gmail.com

AddToAny